Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

2 Wakorinto 11 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Ingekuwa heri muvumilie kidogo masemi yangu ya upumbafu! Ninawaomba kweli munivumilie!

2 Mimi ninasikia wivu kwa ajili yenu sawa vile Mungu anavyousikia vilevile. Kwa maana ninyi ni kama binti mukamilifu niliyemwowesha kwa mume mumoja, ndiye Kristo.

3 Lakini ninaogopa kwamba sawa vile nyoka alivyomudanganya Eva kwa werevu wake, mawazo yenu vilevile yasipotoshwe hata mupate kupoteza uaminifu na ukamilifu wenu kwa Kristo.

4 Hii inatokana na kuona jinsi munavyomukubali mutu yeyote anayekuja kwenu na kuwahubiri habari za Yesu mwingine asiyekuwa yule sisi tuliyemuhubiri. Na zaidi ya hii munakubali upesi kupokea roho ingine na ujumbe mwingine vinavyokuwa tofauti na Roho au Habari Njema muliyopokea toka kwetu.

5 Ninazani kwamba wale mitume wanaohesabiwa kuwa wakubwa zaidi hawanipiti kitu kabisa.

6 Inaonekana kuwa mimi si mutu anayeelewa kusema, lakini kwa ngambo ya elimu, mimi ninaielewa sana. Nasi tumeonyesha hayo yote kila wakati na katika mambo yote.

7 Mimi niliwatangazia Habari Njema ya Mungu bila kudai mushahara. Nilijinyenyekeza kusudi mupate kutukuzwa. Basi kwa kujinyenyekeza vile, nilifanya kosa?

8 Nilipokuwa nikitumika kati yenu nililipwa na makanisa mengine. Ni kama vile nilinyanganya mali ya makanisa yale na kuitumia kwa kuwasaidia.

9 Wakati nilipokuwa kwenu, sikumulemea mutu yeyote nilipohitaji kitu fulani, kwa maana wandugu waliotoka Makedonia waliniletea vitu vyote nilivyohitaji. Nilijiangalia vizuri katika mambo yote kusudi nisiwalemee, nami nitaendelea kujiangalia vema.

10 Kufuatana na vile ninavyosema ukweli kama vile Kristo, ninaapa kwamba hakuna anayeweza kunizuiza kujivuna juu ya jambo hilo katika jimbo lote la Akaya.

11 Kwa sababu gani ninasema hivi? Kwa sababu siwapendi? Hapana, Mungu anajua kwamba ninawapenda.

12 Nitaendelea kufanya sawasawa ninavyofanya kwa sasa, kusudi niwafungie njia zote wale wanaotafuta kujivuna kwamba wanatumika sawa sisi.

13 Watu wale ni mitume wa uongo, wanafanya kazi yao kwa udanganyifu wakijisingizia kuwa mitume wa kweli wa Kristo.

14 Na jambo hilo si la kushangaza kwa maana Shetani mwenyewe anajisingizia kuwa malaika wa mwangaza.

15 Basi si jambo la ajabu kama watumishi wake vilevile wanajigeuza kuwa watumishi wa haki. Kwa mwisho wao watalipwa kufuatana na matendo yao.


Paulo anavumilia mateso yake ya kitume

16 Mimi ninasema tena: mutu asinizanie kuwa mupumbafu. Kama si vile, basi munihesabu kama mupumbafu, kusudi nami nipate kujivuna kidogo vilevile.

17 Maneno haya ninayosema sasa hayafuatani na mapenzi ya Bwana, lakini ninayasema tu kama mupumbafu kuelekea jambo hili la kujivuna.

18 Watu wengi wanajivuna kwa namna ya kimwili, kwa sababu hiyo mimi nitajivuna vilevile.

19 Ninyi munajidai kuwa wenye hekima na ndiyo maana munapenda kuwavumilia wapumbafu!

20 Munavumilia hata mutu anayewatia katika utumwa, anayeiba mali zenu, anayewagandamiza, anayewazarau na anayewapiga kofi kwenye uso.

21 Ninasikia haya ya kuisema: tumekuwa zaifu kwa kufanya vile! Lakini kama watu wengine wanasubutu kujivuna juu ya kitu chochote, mimi vilevile nitajivuna. Sasa ninasema kama vile mupumbafu.

22 Watu wale ni Waebrania? Mimi vilevile. Wao ni Waisraeli? Mimi vilevile. Wao ni wa uzao wa Abrahamu? Mimi vilevile.

23 Sasa nitasema kama mwenda-wazimu: wao ni watumishi wa Kristo? Mimi ni mutumishi wake zaidi kuliko wao. Nimetumika kazi nyingi zaidi, nimefungwa mara nyingi zaidi, nimepigwa zaidi, na mara nyingi nimekuwa katika hatari ya kufa.

24 Mara tano Wayuda wamenipiga viboko makumi tatu na tisa.

25 Waroma wamenipiga fimbo mara tatu na mara moja walitaka kuniua kwa kunitupia mawe. Mara tatu chombo nilichosafiri nacho kilizama kwa kuvunjika. Mara moja, nilishinda ndani ya bahari kwa muda wa siku nzima.

26 Katika safari zangu nyingi nimepata hatari ya mafuriko ya mito, hatari ya wanyanganyi, hatari kutoka kwa wanainchi wenzangu na kutoka kwa watu wa mataifa mengine. Nilikuwa katika hatari ndani ya miji, katika jangwa, katika bahari na kati ya wandugu za uongo.

27 Nimesumbuka kwa kufanya kazi ngumu, nimepata magumu, nimekesha mara nyingi. Mara nyingi niliteswa na njaa na kiu; mara nyingi nililazimishwa kutokula. Nimeteseka na baridi na ukosefu wa nguo.

28 Na bila kutaja mambo yote mengine kama hayo, kila siku ninashugulika na makanisa yote.

29 Kukiwa mutu anayepatwa na uzaifu, mimi ninajisikia muzaifu vilevile. Kukiwa mutu anayeanguka katika zambi, ninasikia uchungu.

30 Kama ikinipasa kujivuna nitajivuna kwa ajili ya uzaifu wangu.

31 Mungu Baba ya Bwana Yesu, anayetukuzwa hata milele, anajua kwamba sisemi uongo.

32 Wakati nilipokuwa Damasiki, liwali wa mufalme Areta aliweka walinzi katika muji ule kusudi wanikamate.

33 Lakini wakanitia ndani ya kitunga na kunishusha kwenye ukuta wa muji, tokea ndani ya dirisha, nami nikapata kuponyoka.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan