2 Wakorinto 10 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Sasa mimi Paulo mwenyewe ninawaomba kwa upole na kwa wema sawa na ule wa Kristo; mimi yule ambaye wanasema juu yake kwamba ni mupole wakati ninapokuwa pamoja nanyi, lakini ni mukali wakati ninapokuwa mbali nanyi. 2 Ninawasihi kwamba nitakapofika kwenu, musinisukume kuwa mukali. Kwa maana nina uhakika kwamba nitawatendea vile wale watu wote wanaozania kwamba sisi tunaishi maisha ya kimwili. 3 Kwa maana ijapokuwa tunaishi katika dunia, lakini hatufanyi vita kwa namna ya kimwili. 4 Silaha tunazotumia katika vita si za kimwili, lakini silaha zetu ni uwezo wa Mungu unaoweza kuharibu upango wa adui. Tunaharibu mawazo ya uongo na 5 kuangusha vizuizo vyote watu wanavyojivunia kwa kupinga elimu ya Mungu. Tunatawala mafikiri ya watu na kuyafanya yapate kumutii Kristo. 6 Sisi tuko tayari kuazibu kila kitendo cha uasi, mutakapoonyesha kwamba munatii kabisa. 7 Ninyi munaangalia tu namna vitu vinavyoonekana kwa inje. Mutu yeyote anayejiaminia kwamba yeye ni wa Kristo, inafaa afikiri tena yeye mwenyewe mambo haya: ikiwa yeye ni wa Kristo sisi vilevile ni wa Kristo. 8 Kwa maana sioni haya hata kama nimejivuna zaidi kwa ajili ya uwezo Bwana aliotupatia sisi. Kwa maana uwezo ule ni kwa ajili ya kuwajenga katika imani, lakini si wa kubomoa. 9 Sitaki kuonekana kwamba ninataka kuwaogopesha kwa barua zangu. 10 Kwa sababu wengi wanasema: “Barua za Paulo ni kali na zenye maneno mazito; lakini yeye mwenyewe anapokuwa katikati yetu ni muzaifu na namna yake ya kusema ni ya kuzarauliwa.” 11 Inafaa mutu yule anayesema vile ajue vema kwamba hakuna tofauti kati ya maneno tunayoandika katika barua zetu wakati tunapokuwa mbali, na yale tutakayofanya wakati tutakapokuwa pamoja nanyi. 12 Kwa kweli hatungesubutu kujifananisha au kujilinganisha na watu wale wanaojisifu wenyewe. Wao ni wapumbafu. Wanajipima kufuatana na kipimo chao wenyewe na kujilinganisha na wao wenyewe. 13 Sisi hatutajivuna kupita kipimo, lakini tunataka kutumia kile kipimo cha kazi ile Mungu aliyotupatia na iliyotufikisha vilevile mpaka kwenu. 14 Hatutambuki mipaka yetu sawa vile hatukufika kwenu. Kwa maana tulifika kwenu, tukiwatangazia Habari Njema ya Kristo. 15 Basi, hatujivuni kupita kipimo juu ya kazi ya watu wengine. Lakini tunatumaini kwamba imani yenu itakapokuwa ikiongezeka, tutaweza kufanya kazi kubwa zaidi kati yenu kufuatana na kipimo cha kazi tuliyopewa na Mungu. 16 Kisha tutaweza kuhubiri Habari Njema katika inchi zinazokuwa mbali kupita inchi yenu, kuliko kujisifu juu ya kazi watu wengine waliyokwisha kufanya kufuatana na kipimo walichopewa. 17 Lakini, kama Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Anayetaka kujivuna, ajivune kwa ajili ya Bwana.” 18 Kwa maana, mutu anayekubaliwa si yule anayejisifu mwenyewe, lakini ni yule anayesifiwa na Bwana. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo