Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

2 Wafalme 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Shoka linapatikana

1 Siku moja, wanafunzi wa manabii walimulalamikia Elisha wakisema: “Pahali hapa tunapokaa ni padogo sana kwetu!

2 Uturuhusu tuende Yordani tukate kila mutu muti mumoja kusudi tujijengee pahali pa kututoshelea.” Elisha akawajibu: “Mwende.”

3 Mumoja wao akamwomba akisema: “Tafazali ninakusihi uende pamoja na watumishi wako.” Naye akajibu: “Nitakwenda.”

4 Hivyo akaenda pamoja nao, na walipofika kwenye muto Yordani wakaanza kukata miti.

5 Mumoja wao alipokuwa anakata miti, shoka lake likachomoka na kuanguka ndani ya maji. Akalia, akisema: “Sasa bwana wangu nitafanya nini? Shoka hili tulikuwa tumeliazima!”

6 Elisha akauliza: “Liliangukia wapi?” Mutu huyo akamwonyesha. Elisha akakata kijiti na kukitupa ndani ya maji na palepale shoka likaelea juu ya maji.

7 Elisha akamwamuru alikamate naye akanyoosha mukono, akalikamata.


Waaskari wa Waaramu wanashindwa

8 Wakati mumoja kulikuwa vita kati ya Aramu na Israeli. Basi, mufalme wa Aramu akafanya shauri na wakubwa wa waaskari wake juu ya pahali watakapopiga kambi.

9 Lakini Elisha akamupelekea mufalme wa Israeli habari afanye angalisho na pahali pale, kwa sababu Waaramu walikuwa tayari kupashambulia.

10 Basi, mufalme wa Israeli akapeleka waaskari wake karibu na pahali alipoambiwa. Elisha aliendelea kumwonya mufalme naye mufalme alijiweka katika hali ya angalisho. Jambo hilo lilifanyika mara nyingi.

11 Mufalme wa Aramu akafazaishwa sana na hali hiyo. Akawaita wakubwa wa waaskari wake, akawauliza: “Muniambie ni nani kati yenu anayekuwa upande wa mufalme wa Israeli?”

12 Mumoja wao akajibu: “Hakuna anayekuwa upande wake, ee mufalme. Anayefanya vile ni Elisha, nabii anayekuwa kule Israeli. Yeye anamwambia mufalme wa Israeli mambo yote unayosema hata ukiwa katika chumba chako cha kulala.”

13 Mufalme akawaambia: “Mwende mupeleleze mujue pahali anapokuwa nami nitawatuma watu wamukamate.” Basi, wakamwambia kwamba Elisha alikuwa kule Dotani.

14 Kwa hiyo mufalme akatuma kule kundi kubwa la waaskari pamoja na farasi na magari ya vita. Kundi hilo likafika kule wakati wa usiku na kuuzunguka muji.

15 Mutumishi wa Elisha alipoamuka mapema kesho yake na kutoka inje, akaona waaskari pamoja na farasi na magari ya vita wameuzunguka muji. Akarudi ndani akasema: “Ole wetu, ee, Bwana wangu! Sasa tutafanya nini?”

16 Elisha akamujibu: “Usiogope kwa sababu wanaokuwa pamoja nasi ni wengi kuliko wanaokuwa pamoja nao.”

17 Kisha Elisha akaomba: “Ee Yawe, umufumbue macho kusudi apate kuona!” Basi, Yawe akamufumbua macho yule kijana, akaona farasi na magari ya moto yakiwa kila pahali katika mulima wote, kumuzunguka Elisha.

18 Waaramu waliposhambulia, Elisha alimwomba Yawe akisema: “Ninakuomba ufanye watu hawa wakuwe vipofu!” Yawe akasikiliza ombi lake na kuwafanya vipofu.

19 Halafu Elisha akawaendea na kuwaambia: “Mumepotea njia. Huu siyo muji ambao munautafuta. Munifuate nami nitawapeleka kwa yule munayemutafuta.” Naye akawaongoza mpaka Samaria.

20 Mara tu walipoingia katika muji, Elisha akaomba, akisema: “Ee Yawe, uwafumbue macho kusudi waone.” Yawe akasikia ombi lake, akawafumbua macho. Nao wakajikuta wako katikati ya muji wa Samaria.

21 Mufalme wa Israeli alipowaona Waaramu, alimwuliza Elisha: “Niwaue?”

22 Elisha akajibu: “Hapana, usiwaue. Maana hawa unaotaka kuwaua uliwateka kwa upanga wako na mushale wako? Uwape chakula na maji, wakule na kunywa kisha uwaache warudie kwa bwana wao.”

23 Mufalme wa Israeli akawafanyia karamu kubwa. Walipomaliza kula na kunywa, akawarudisha kwa bwana wao. Toka wakati ule, Waaramu hawakuishambulia tena inchi ya Israeli.


Muji wa Samaria unazungukwa kwa vita

24 Nyuma ya hayo, mufalme Beni-Hadadi wa Aramu akakusanya waaskari wake wote akatoka na kuuzunguka muji wa Samaria.

25 Matokeo yake ilikuwa njaa kali katika muji wa Samaria. Kichwa cha punda kilinunuliwa kwa vikoroti makumi tatu vya feza, na grama mia moja za mavi ya njiwa zilinunuliwa kwa vikoroti vitano vya feza.

26 Siku moja mufalme wa Israeli alipokuwa anatembea juu ya ukuta wa muji, alisikia mwanamuke mumoja akimwita: “Unisaidie, ee bwana wangu mufalme!”

27 Mufalme akamwambia: “Yawe asipokusaidia, mimi nitaweza kukupa musaada kutoka wapi? Kutoka katika kiwanja cha kupepetea ngano au kutoka katika kikamulio?

28 Shida yako ni nini?” Akamujibu: “Juzi mwanamuke huyu alinishauria tumukule mwana wangu na kesho yake tutamukula wake.

29 Tukamupika mwana wangu, tukamukula. Kesho yake nikamwambia tumukule mwana wake, lakini alikuwa amemuficha!”

30 Mara mufalme aliposikia maneno ya mwanamuke yule alipasua nguo zake kwa huzuni, na watu waliokuwa karibu na ukuta waliona kwamba alikuwa amevaa nguo ya gunia ndani yake.

31 Naye akasema: “Mungu aniue Elisha mwana wa Safati asipokatwa kichwa leo!”

32 Halafu akatuma mujumbe kwenda kumuleta Elisha. Wakati uleule, Elisha alikuwa ndani ya nyumba pamoja na wazee waliomutembelea. Mbele ya kufika kwa mujumbe wa mufalme, Elisha akawaambia wazee: “Yule mwuaji amemutuma mutu kuja kunikata kichwa! Atakapofika hapa, mufunge mulango, wala musimuruhusu aingie. Vilevile bwana wake anamufuata nyuma.”

33 Mbele hata hajamaliza kusema, mufalme akafika, akasema: “Mabaya haya yametoka kwa Yawe! Nitangojea nini tena kutoka kwake?”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan