2 Wafalme 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Elisha anamusaidia mujane masikini 1 Basi, mwanamuke mumoja kati ya wake za wanafunzi wa manabii akamwendea Elisha, akamwambia: “Mutumishi wako, mume wangu amekufa, na kama vile unavyojua, alikuwa mwenye kumwogopa Mungu. Lakini mutu aliyemukopesha feza amekuja kuwatwaa wana wangu wawili wakuwe watumwa wake.” 2 Elisha akamwuliza: “Sasa nikusaidie namna gani? Uniambie kile unachokuwa nacho kwako.” Mama yule mujane akamujibu: “Mimi mutumishi wako sina kitu chochote lakini chupa ndogo ya mafuta.” 3 Elisha akamwambia: “Kwenda kwa jirani zako, uazime vyombo vitupu vingi vya kutosha. 4 Kisha uende, wewe pamoja na wana wako, mujifungie ndani ya nyumba, na muanze kujaza mafuta. Kila chombo munachojaza, mukiweke pembeni.” 5 Akaenda na kujifungia ndani ya nyumba na wana wake na kuanza kumimia mafuta ndani ya vyombo. 6 Vilipojaa vyote, akamwambia mwana wake mumoja: “Uniletee chombo kingine.” Mwana wake akamujibu: “Vyote vimejaa!” Hapo mafuta yakakoma kutiririka. 7 Akarudi kwa mutu wa Mungu na kumweleza habari hiyo. Naye mutu wa Mungu akamwambia: “Kwenda uuzishe hayo mafuta na kulipa madeni yako, ndipo wewe na wana wako mutaishi kwa kutumia hayo yatakayobaki.” Elisha na mama tajiri Musunami 8 Siku moja Elisha alikwenda Sunemu, ambako kulikuwa mama mumoja tajiri. Mama yule akamwalika Elisha kwa chakula, na toka siku hiyo ikakuwa kawaida Elisha kula chakula kwake kila mara alipopitia kule. 9 Mama yule akamwambia mume wake: “Sina shaka kwamba mutu huyu anayefika kwetu kila mara ni mutakatifu wa Mungu. 10 Ninakuomba basi tumujengee chumba na kule tumwekee kitanda, meza, kiti na taa, kusudi akitumie kila mara anapotutembelea.” 11 Siku moja Elisha akafika kule na kuingia ndani ya chumba chake kusudi apumzike. 12 Akamwambia mutumishi wake Gehazi: “Umwite yule mama Musunami.” Alipomwita akakuja na kusimama mbele yake. 13 Naye Elisha akamwambia Gehazi: “Umwambie, tumeona jinsi alivyotushugulikia; sasa anataka tumutendee jambo gani? Angependa aombewe lolote kwa mufalme au kwa jemadari wa waaskari?” Mama Musunami akamujibu: “Mimi ninaishi kati ya watu wangu.” 14 Elisha akasema: “Tumufanyie nini basi?” Gehazi akamujibu: “Hakika hana mutoto, na mume wake amekuwa muzee.” 15 Elisha akamwambia: “Umwite.” Naye akamwita. Akakuja na kusimama kwenye mulango. 16 Elisha akamwambia: “Mwaka kesho, kwa wakati kama huu, utakuwa na mutoto katika mikono yako.” Mama akamujibu: “Hapana, Bwana wangu! Wewe ni mutu wa Mungu; usinidanganye mimi mutumishi wako!” 17 Lakini yule mwanamuke akapata mimba na kuzaa mutoto wakati kama ule mwaka uliofuata, kama vile Elisha alivyokuwa amemwambia. 18 Mutoto yule alipokomaa, alitoka siku moja pamoja na baba yake akafuatana na wavunaji, 19 naye akamwambia baba yake: “Ole, kichwa changu! Ninaumwa na kichwa!” Baba yake akamwambia mutumishi wake mumoja: “Umupeleke kwa mama yake.” 20 Alipofikishwa kwa mama yake, aliikaa juu ya magoti ya mama yake mpaka saa sita za muchana, halafu akakufa. 21 Mama yake akamupeleka na kumulalisha kwenye kitanda cha mutu wa Mungu, akaufunga mulango na kuondoka. 22 Akamwita mume wake na kumwambia: “Unipe mutumishi mumoja na punda mumoja, kusudi nimwendee mara moja yule mutu wa Mungu, kisha nitarudi.” 23 Mume wake akamwuliza: “Kwa nini unataka kumwona leo? Leo si sikukuu ya mwandamo wa mwezi wala Sabato.” Akamujibu: “Si neno.” 24 Akatandika punda na kumwambia mutumishi: “Sasa kaza mwendo, wala usipunguze mpaka nitakapokuambia.” 25 Basi, akaondoka, akaenda mpaka kwenye mulima Karmeli kule mutu wa Mungu alipokuwa. Mutu wa Mungu alipomwona akikuja, akamwambia Gehazi mutumishi wake: “Angalia, ninamwona Musunami akikuja. 26 Kimbia mara moja kumupokea na kumwuliza: ‘Uko muzima? Mume wako ni muzima? Mutoto ni muzima?’ ” Naye Musunami akamujibu: “Tuko wazima.” 27 Alipofika kwenye mulima kwa mutu wa Mungu, akamushika miguu, naye Gehazi akakaribia kusudi amwondoe. Lakini mutu wa Mungu akamwambia: “Umwache, maana ana uchungu mukali, naye Yawe hakunijulisha jambo hilo.” 28 Huyo mama akamwambia: “Bwana wangu, mimi nilikuomba mutoto? Sikukusihi kwamba usinipatie matumaini ya uongo?” 29 Elisha akamwambia Gehazi: “Ujitayarishe kusafiri, twaa fimbo yangu, na uende mara moja. Usisimame katika njia kwa kumusalimia mutu yeyote, na mutu yeyote akikusalimia katika njia, usipoteze wakati kwa kumurudishia salamu. Kwenda moja kwa moja mpaka katika nyumba na kuweka fimbo yangu juu ya uso wa mutoto.” 30 Mwanamuke akamwambia Elisha: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.” Basi Elisha akaondoka na kufuatana naye. 31 Gehazi akatangulia mbele, na alipofika akaweka fimbo ya Elisha juu ya uso wa mutoto, lakini hakukuonekana kitambulisho chochote cha uzima. Akarudi na kukutana na Elisha, akamwambia: “Kijana hakuamuka.” 32 Elisha alipofika, akaingia peke yake ndani ya chumba na kuona maiti ya kijana kwenye kitanda. 33 Basi, akafunga mulango na kumwomba Yawe. 34 Halafu akajilaza juu ya mutoto, kinywa chake juu ya kinywa cha mutoto, na macho yake juu ya macho ya mutoto na mikono yake juu ya mikono ya mutoto. Na alipokuwa amekaa hivyo, mwili wa mutoto ukaanza kupata joto. 35 Elisha akasimama na kutembeatembea ndani ya chumba, kisha akarudi na kujilaza tena juu ya mutoto. Mutoto akapiga chafya mara saba, halafu akafungua macho. 36 Elisha akamwita Gehazi na kumwambia: “Umwite yule Musunami.” Alipoitwa Elisha akamwambia: “Kamata mwana wako.” 37 Akainama kwenye miguu ya Elisha kwa shukrani na kumukamata mwana wake. Miujiza mingine miwili ya Elisha 38 Elisha akarudi Gilgali wakati katika inchi kulikuwa njaa. Siku moja, alipokuwa akifundisha wanafunzi wa manabii alimwambia mutumishi wake: “Weka chungu kikubwa juu ya moto, uwapikie manabii chakula.” 39 Mumoja wao akaenda katika shamba na kuchuma mboga. Kule akaona mboga za pori, akachuma mboga nyingi kwa kadiri alivyoweza kubeba. Akakuja nazo, akazikatakata na kuzitia ndani ya chungu bila kuzijua. 40 Chakula kikapakuliwa. Lakini walipokionja wakamulilia Elisha wakisema: “Ee mutu wa Mungu, chakula hiki kitatuua!” Nao hawakuweza kukikula. 41 Elisha akaagiza aletewe unga. Akaletewa unga, naye akautia ndani ya chungu na kusema: “Sasa uwape chakula wakule.” Wakakikula, na hapo hakikuwazuru. 42 Mutu mumoja akatoka Bali-Salisa, akamuletea Elisha mikate makumi mbili iliyotengenezwa kwa shayiri ya malimbuko ya mavuno ya mwaka ule na masuke mabichi ya ngano katika gunia. Elisha akamwagiza Gehazi awape watu wakule. 43 Mutumishi wake akasema: “Sitawapa kwa sababu hakitawatosha watu mia moja”. Elisha akasema: “Uwape wakule, kwa sababu Yawe amesema kwamba watakula na kushiba na kingine kitabaki.” 44 Mutumishi wake akawatayarishia chakula, wakakula na kushiba, na kingine kikabaki, kama vile Yawe alivyosema. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo