2 Wafalme 25 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maangamizi ya Yerusalema ( 2 Sik 36.13-21 ; Yer 52.3b-11 ) 1 Katika siku ya kumi ya mwezi wa kumi, mwaka wa tisa wa utawala wa Zedekia, Nebukadneza mufalme wa Babeli akafika na waaskari wake kwa kushambulia Yerusalema. Akapiga kambi mbele ya muji ule na kujenga ngazi kuuzunguka. 2 Muji uliendelea kuzungukwa mpaka mwaka wa kumi na moja wa utawala wa Zedekia. 3 Katika siku ya tisa ya mwezi wa ine njaa ilikuwa kali sana katika muji hata hakukuwa chakula chochote kwa ajili ya wakaaji wake. 4 Basi, sehemu ya ukuta wa muji ukabomolewa, naye mufalme pamoja na waaskari wote wakakimbia wakati wa usiku wakipitia katika bustani ya mufalme kwenye mulango katikati ya kuta mbili, wakaenda upande wa Araba, ingawa Wababeli walikuwa wameuzunguka muji. 5 Lakini waaskari wa Babeli wakamufuata mufalme na kumuteka kwenye bonde za Yeriko, nao waaskari wake wote wakamwacha, wakatawanyika. 6 Basi, Wababeli wakamuteka mufalme, wakamupeleka kwa mufalme wao kule Ribla, naye akamuhukumu. 7 Halafu wakawaua wana wa Zedekia mbele yake, kisha wakamwongoa macho yake. Kwa mwisho wakamufunga kwa minyororo, wakamupeleka Babeli. Hekalu linateketezwa ( Yer 52.12-23 ) 8 Katika siku ya saba ya mwezi wa tano wa mwaka wa kumi na tisa wa utawala wa Nebukadneza mufalme wa Babeli, Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme, akaingia Yerusalema. 9 Akaichoma kwa moto nyumba ya Yawe, nyumba ya kifalme na nyumba zote za Yerusalema; kila nyumba kubwa akaichoma kwa moto. 10 Nao waaskari wote wa Babeli waliokuwa pamoja na mukubwa wa waaskari na walinzi wa mufalme walizibomoa kuta zilizouzunguka Yerusalema. 11 Nebuzaradani, mukubwa wa waaskari wa mufalme, akawapeleka katika uhamisho watu waliokuwa wamebakia katika muji na wale wote waliokuwa wamejitoa wenyewe kwa mufalme wa Babeli pamoja na watu wengine wote. 12 Lakini aliacha wamoja wa watu waliokuwa wamasikini kabisa katika inchi. Aliwaacha watunze mizabibu na kulima mashamba. 13 Wababeli walivunja vipandevipande nguzo za shaba ambazo zilikuwa katika nyumba ya Yawe, pamoja na viikalio vya birika kubwa la shaba nyeusi lililokuwa mule katika nyumba ya Yawe, wakapeleka shaba nyeusi mpaka Babeli. 14 Vilevile walipeleka vyungu, majembe, makasi na miiko iliyotumiwa kwa kuchoma ubani na vyombo vingine vyote vya shaba nyeusi vilivyotumiwa katika kazi ya hekalu, 15 wakapeleka vyetezo na mabakuli. Mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme akapeleka mbali kila chombo cha zahabu na kila chombo cha feza. 16 Shaba yote nyeusi Solomono aliyotumia kwa kutengeneza zile nguzo mbili, birika lile kubwa na viikalio kwa ajili ya nyumba ya Yawe haikuweza kupimwa kwa uzito. 17 Kila nguzo ilikuwa na urefu wa metre nane, na juu yake kulikuwa kichwa cha shaba nyeusi. Urefu wa kila kichwa ulikuwa metre moja na sentimetre makumi mbili na tano. Kila kichwa kilizungushiwa mapambo ya makomamanga, yote ya shaba nyeusi. Watu wa Yuda wanapelekwa Babeli ( Yer 52.24-27 ) 18 Kisha Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme akamupeleka Seraya, Kuhani Mukubwa, kuwa mufungwa pamoja na Zefania, kuhani wa pili, na wakubwa wa walinda milango watatu. 19 Akamupeleka jemadari mumoja kule katika muji ambaye alikuwa akiwaongoza waaskari katika vita, pamoja na watu watano wenye heshima wa mufalme ambao aliwakuta kule. Vilevile, akamupeleka katibu wa jemadari wa waaskari ambaye alichunga habari za kuandika waaskari wapya pamoja na watu makumi sita wenye heshima ambao aliwakuta Yerusalema. 20 Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi akawatwaa watu hao, akawapeleka kwa mufalme wa Babeli kule Ribla. 21 Mufalme Nebukadneza wa Babeli akawapiga na kuwaua watu hao kule Ribla katika inchi ya Hamati. Hivyo watu wa Yuda wakapelekwa kuwa watumwa inje ya inchi yao. Gedalia, liwali wa Yuda ( Yer 40.7-9 ; 41.1-3 ) 22 Mufalme Nebukadneza wa Babeli akamuchagua Gedalia mwana wa Ahikamu, mujukuu wa Safanu, kuwa mutawala wa watu wote wa Yuda ambao hawakupelekwa Babeli. 23 Kisha wakubwa wote wa waaskari pamoja na watu wao waliposikia kwamba mufalme wa Babeli alimuchagua Gedalia kuwa mutawala, wakamwendea Gedalia kule Mispa. Watu hao walikuwa ni: Isimaeli mwana wa Netania, Yohana mwana wa Karea, Seraya mwana wa Taumeti wa muji wa Netofati, na Yazania mwana wa Mumakati. 24 Naye Gedalia aliapa mbele yao na watu wao, akasema: “Musiogope kwa sababu ya wakubwa wa Wababeli. Mukae katika inchi mumutumikie mufalme wa Babeli na mambo yote yatawaendekea vema.” 25 Katika mwezi wa saba, Isimaeli mwana wa Netania, mujukuu wa Elisama, aliyekuwa wa ukoo wa kifalme, akafika kwa Gedalia pamoja na watu kumi, akamushambulia Gedalia, akamwua. Vilevile, akawaua Wayuda na Wababeli waliokuwa naye. 26 Halafu, Waisraeli wote, wadogo na wakubwa pamoja na wakubwa wa waaskari wakaondoka, wakaenda Misri, kwa sababu waliwaogopa Wababeli. Yoyakini anaachiliwa ( Yer 52.31-34 ) 27 Katika mwaka wa makumi tatu na mbili, Ewili-Merodaki mufalme wa Babeli alianza kutawala. Mwaka uleule akamusamehe Yoyakini mufalme wa Yuda, akamufungua. Hayo yalitokea katika siku ya makumi mbili na saba ya mwezi wa kumi na mbili wa mwaka wa makumi tatu na saba tangu Yoyakini alipopelekwa katika uhamisho. 28 Aliongea naye vizuri na kumupa nafasi ya heshima kuliko wafalme wengine waliokuwa pamoja naye kule Babeli. 29 Basi, Yoyakini akabadilisha nguo zake za mufungwa. Kila siku alikuwa anapata chakula chake kwa mufalme siku zote za maisha yake. 30 Alipatiwa na mufalme posho yake siku kwa siku, kwa muda wa maisha yake yote kufuatana na mahitaji yake. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo