2 Wafalme 22 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mufalme Yosia wa Yuda ( 2 Sik 34.1-2 ) 1 Yosia alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala akiwa kule Yerusalema na utawala wake ulidumu kwa miaka makumi tatu na mumoja. Mama yake aliitwa Yedida, binti wa Adaya mukaaji wa muji wa Bozikati. 2 Yosia alitenda kwa usawa mbele ya Yawe. Alifuata mienendo yote ya babu yake Daudi; hakuiacha hata kidogo. Kitabu cha sheria kinaonekana ( 2 Sik 34.8-28 ) 3 Katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wake, mufalme alimutuma Safanu mwana wa Azalia, mujukuu wa Mesulamu, mwandishi katika nyumba ya Yawe akisema: 4 “Kwenda kwa Kuhani Mukubwa Hilkia kusudi ahesabu feza zilizoletwa katika nyumba ya Yawe, ambazo walinzi wa mulango walizikusanya kutoka kwa watu; 5 nazo zitolewe kwa wale wanaosimamia kazi ya kutengeneza vizuri nyumba ya Yawe kusudi wapate kuwalipa wafundi wanaofanya kazi ya kutengeneza mabomoko, 6 waseremala, wajengaji na watumishi wengine wenye kujenga, na kununua mbao na mawe yaliyochongwa kwa ajili ya kutengeneza nyumba. 7 Watu wanaosimamia ujenzi wasiombwe kutoa hesabu ya matumizi ya feza watakazopewa, kwa sababu wanazitumia kwa uaminifu.” 8 Kisha Kuhani Mukubwa Hilkia akamwambia Safanu, mwandishi: “Nimekipata kitabu cha Sheria katika nyumba ya Yawe.” Halafu Hilkia akamupatia Safanu kitabu, naye akakisoma. 9 Mwandishi Safanu akamwendea mufalme na kutoa habari, akisema: “Watumishi wako wametoa feza zilizopatikana katika nyumba, halafu wakazipeleka kwa wafundi wanaosimamia kazi ya kutengeneza nyumba ya Yawe.” 10 Kisha Safanu, mwandishi akamwambia mufalme: “Kuhani Hilkia amenipa kitabu.” Naye Safanu akakisoma mbele ya mufalme. 11 Mufalme aliposikia maneno ya Kitabu cha Sheria, akapasua nguo zake. 12 Akaamuru kuhani Hilkia, Ahikamu mwana wa Safanu na Akibori mwana wa Mikaya pamoja na mwandishi Safanu na Asaya mutumishi wa mufalme, akisema: 13 “Mwende muombe shauri kutoka kwa Yawe kwa ajili yangu, na kwa watu wa Yuda wote juu ya maneno ya kitabu hiki kilichopatikana kwa sababu kasirani ya Yawe imewaka juu yetu, maana babu zetu hawakutii maneno ya kitabu hiki na kutimiza yote yaliyoandikwa juu yetu.” 14 Kwa hiyo kuhani Hilkia, Ahikamu, Akibori, Safanu na Asahiya, wote walikwenda kuomba shauri kwa mwanamuke mumoja nabii jina lake Hulda aliyekuwa muke wa Salumu mwana wa Tikwa, mujukuu wa Harihasi, mutunza nguo za hekalu. Wakati ule, Hulda alikuwa anaishi katika mutaa wa pili wa Yerusalema, nao wakazungumuza naye. 15 Basi akawaambia: “Hivi ndivyo Yawe, Mungu wa Israeli, anavyosema: Mumwambie yule aliyewatuma kwangu, 16 Yawe anasema hivi: Nitaleta uovu juu ya pahali hapa na juu ya wakaaji wake kama vile inavyokuwa katika kitabu kilichosomwa na mufalme wa Yuda. 17 Kwa sababu wameniacha na kufukizia miungu mingine ubani kusudi watu wanikasirikishe kwa kazi zote za mikono yao, basi, kasirani yangu juu ya Yerusalema itawaka na haitaweza kutulizwa. 18 Lakini juu ya mufalme wa Yuda aliyewatuma kuomba shauri la Yawe, mumwambie kwamba, hivi ndivyo Yawe, Mungu wa Israeli anavyosema juu ya maneno uliyoyasikia. 19 Wakati uliposikia niliyosema juu ya pahali hapa na juu ya wakaaji wake, kwamba watakuwa ukiwa na kulaaniwa, ulijuta na kunyenyekea mbele yangu, hata ukapasua nguo yako na kulia mbele yangu. Basi, nami vilevile nimekusikia. 20 Kwa hiyo, nitakukusanya pamoja na babu zako nawe utazikwa katika kaburi kwa amani, macho yako hayataona uovu nitakaoleta juu ya pahali hapa.” Basi wajumbe wakamuletea mufalme Yosia habari hii. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo