Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

2 Wafalme 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Elia ananyanyuliwa mbinguni

1 Wakati ulifika ambapo Yawe alitaka kumupandisha Elia mbinguni katika upepo wa kuzungukazunguka. Elia na Elisha walikuwa katika njia, wakitoka Gilgali.

2 Walipokuwa katika njia, Elia akamwambia Elisha: “Tafazali ubakie hapa. Yawe amenituma niende Beteli.” Lakini Elisha akamwambia: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.” Basi, wakaenda pamoja mpaka Beteli.

3 Wanafunzi wa manabii wa Beteli wakamwendea Elisha, wakamwuliza: “Unajua kwamba leo Yawe atamupeleka bwana wako?” Elisha akajibu: “Ndiyo. Ninajua. Munyamaze.”

4 Kisha Elia akamwambia Elisha: “Tafazali ubakie hapa. Yawe amenituma niende Yeriko.” Lakini Elisha akakataa akisema: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.” Basi, wakaenda pamoja mpaka Yeriko.

5 Wanafunzi wa manabii wa Yeriko wakamwendea Elisha, wakamwuliza: “Unajua kwamba leo Yawe atamupeleka bwana wako?” Elisha akawajibu: “Ndiyo. Ninajua. Munyamaze.”

6 Kisha Elia akamwambia Elisha: “Tafazali ubakie hapa. Yawe amenituma niende Yordani.” Lakini Elisha akasema: “Kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, sitakuacha.” Basi, wakaenda pamoja.

7 Manabii makumi tano wakawafuata mpaka kwenye muto Yordani. Elia na Elisha wakasimama karibu na muto, nao manabii wakasimama mbali kidogo.

8 Elia akavua nguo yake, akaikunja na kupiga nayo maji. Maji yakagawanyika katika sehemu mbili, nao wakavuka mpaka ngambo, wakipitia pahali pakavu.

9 Walipofika ngambo, Elia akamwambia Elisha: “Uniambie jambo unalotaka nikufanyie mbele sijaondolewa kwako.” Elisha akamwambia: “Ninaomba sehemu mara mbili ya roho yako.”

10 Elia akajibu: “Ombi lako ni gumu. Hata hivyo, ikiwa utaniona wakati nitakapoondolewa kwako, itafanyika vile kwako. Lakini usiponiona, basi haitafanyika vile.”

11 Walipokuwa wanatembea na kuongea, kwa rafla gari la moto lililokokotwa na farasi wa moto likawatenganisha. Naye Elia akanyanyuliwa mbinguni katika upepo wa kuzungukazunguka.

12 Elisha alipoona tukio hilo, akalia: “Baba yangu, baba yangu! Ulikuwa wa lazima kuliko magari ya Israeli na wapanda-farasi wake!” Basi, Elisha hakumwona tena Elia. Halafu Elisha akashika nguo zake na kuzipasua vipande viwili.

13 Kisha akaokota nguo ya Elia iliyomwangukia, akarudia na kusimama kwenye ukingo wa muto Yordani.

14 Akayapiga maji kwa nguo ya Elia akisema: “Yuko wapi Yawe, Mungu wa Elia?” Alipopiga maji, yakagawanyika sehemu mbili, naye akavuka mpaka ngambo.

15 Wale wanafunzi wa manabii kutoka Yeriko walipomwona, walisema: “Roho wa Elia yuko kwa Elisha.” Basi, wakaenda kumupokea, wakainama mbele yake kwa heshima.

16 Wakamwambia: “Sisi watumishi wako tuko na mashujaa makumi tano. Tafazali, uwaruhusu waende kumutafuta bwana wako. Labda roho wa Yawe amemubeba na kumutupa juu ya mulima fulani au katika bonde.” Elisha akajibu: “Hapana, musiwatume.”

17 Lakini wao walimwuzi sana mpaka akaona haya, akawaambia: “Muwatume.” Hivyo wakawatuma watu makumi tano, wakaenda wakamutafuta kila fasi kwa muda wa siku tatu nao hawakumwona.

18 Kisha wakarudi kwa Elisha aliyekuwa anawangojea kule Yeriko. Elisha akawauliza: “Sikuwaambia musiende?”


Miujiza ya Elisha

19 Kisha watu wa Yeriko wakamwendea Elisha, wakamwambia: “Bwana, kama vile unavyoona, muji huu ni muzuri, lakini maji tunayokuwa nayo ni mabaya na yanasababisha mimba kuharibika.”

20 Elisha akawaambia: “Mutie chumvi ndani ya bakuli jipya, kisha muniletee.” Nao wakamuletea.

21 Elisha akaenda kwenye chemichemi ya maji, akatupa chumvi hiyo ndani na kusema: “Yawe anasema hivi: Nimeyafanya maji haya kuwa yenye kufaa. Tangu sasa hayatasababisha vifo au kutoa mimba.”

22 Na maji hayo yakakuwa ya kufaa mpaka leo, kama vile Elisha alivyosema.

23 Elisha aliondoka Yeriko, akaenda Beteli. Alipokuwa katika njia, vijana wamoja walitoka katika muji, wakaanza kumuzomea wakisema: “Kwenda zako, kwenda zako muzee wa upaa!”

24 Elisha aligeuka, akawaangalia na kuwalaani kwa jina la Yawe. Dubu wawili wakatoka katika pori, wakawararua vijana makumi ine na wawili kati yao.

25 Elisha akaendelea na safari yake mpaka kwenye mulima Karmeli na tokea kule akarudi Samaria.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan