2 Wafalme 15 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mufalme Azaria wa Yuda ( 2 Sik 26.1-23 ) 1 Katika mwaka wa makumi mbili na saba wa kutawala kwa Yeroboamu mufalme wa Israeli, Azaria mwana wa Amazia, mufalme wa Yuda, akaanza kutawala. 2 Alikuwa na umri wa miaka kumi na sita alipoanza kutawala. Alitawala kwa muda wa miaka makumi tano na miwili akiwa kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Yekolia wa Yerusalema. 3 Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe kama vile baba yake Amazia alivyotenda. 4 Hata hivyo, nafasi za kutambikia kwenye milima hazikuharibiwa, na watu waliendelea kutambika na kufukiza ubani pale. 5 Yawe akamwazibu Azaria, akakuwa na ukoma mpaka alipokufa. Alikaa katika nyumba ya pekee na shuguli zake zote za utawala ziliendeshwa na mwana wake Yotamu. 6 Mambo mengine ya Azaria na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. 7 Azaria akakufa na kuzikwa katika makaburi ya wafalme katika muji wa Daudi; na mwana wake Yotamu akatawala kwa pahali pake. Mufalme Zakaria wa Israeli 8 Katika mwaka wa makumi tatu na nane wa utawala wa Azaria mufalme wa Yuda, Zakaria mwana wa Yeroboamu akaanza kutawala Israeli. Akatawala kwa muda wa miezi sita. 9 Naye, kama vile watangulizi wake, alitenda maovu mbele ya Yawe; hakuacha zambi zile za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. 10 Salumu mwana wa Yabesi alimwasi, akamupiga mbele ya watu na kumwua, kisha akatawala kwa pahali pake. 11 Matendo mengine yote ya Zakaria yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. 12 Basi tukio hilo lilitokana na ahadi ya Yawe kwa mufalme Yehu, kusema: “Wazao wako watatawala Israeli mpaka kizazi cha ine.” 13 Katika mwaka wa makumi tatu na tisa wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Salumu mwana wa Yabesi akaanza kutawala Israeli na akatawala akiwa kule Samaria kwa muda wa mwezi mumoja. 14 Menahemu mwana wa Gadi aliondoka Tirza kwenda Samaria, na kule akamupiga Salumu mwana wa Yabesi, kisha akatawala kwa pahali pake. 15 Matendo mengine yote ya Salumu na uasi wake, yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. 16 Menahemu alipokuwa katika njia kutoka Tirza, aliuharibu kabisa muji wa Tapua na kuangamiza wakaaji wake pamoja na inchi yote iliyouzunguka kwa sababu hawakujitoa kwake. Vilevile akapasua tumbo za wanawake wenye mimba. Mufalme Menahemu wa Israeli 17 Katika mwaka wa makumi tatu na tisa wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Menahemu mwana wa Gadi akaanza kutawala Israeli. Akatawala akiwa kule Samaria kwa muda wa miaka kumi. 18 Alitenda maovu mbele ya Yawe. Hakuacha maovu ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. 19 Basi, Puli mufalme wa Asuria akashambulia inchi ya Israeli, naye Menahemu akamupa kilo elfu makumi tatu na ine za feza kusudi amusaidie kuimarisha mamlaka yake juu ya inchi ya Israeli. 20 Menahemu alipata feza hiyo kwa kuwalazimisha watajiri wa Israeli kutoa muchango wa vikoroti makumi tano vya feza kila mumoja. Halafu Puli hakukaa Israeli lakini akarudi katika inchi yake. 21 Mambo mengine ya Menahemu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. 22 Menahemu akakufa, naye mwana wake Pekahia akatawala kwa pahali pake. Mufalme Pekahia wa Israeli 23 Katika mwaka wa makumi tano wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Pekahia mwana wa Menahemu akaanza kutawala Israeli. Akatawala akiwa kule Samaria kwa muda wa miaka miwili. 24 Alitenda maovu mbele ya Yawe; hakuacha zambi za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. 25 Peka mwana wa Remalia, ambaye alikuwa mukubwa wa waaskari wa Pekahia, alishirikiana na watu wengine makumi tano kutoka Gileadi, akamwua Pekahia katika chumba cha ndani cha nyumba ya mufalme kule Samaria na kuwa mufalme kwa pahali pake. 26 Mambo mengine ya Pekahia na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Mufalme Peka wa Israeli 27 Katika mwaka wa makumi tano na mbili wa utawala wa mufalme Azaria wa Yuda, Peka mwana wa Remalia akaanza kutawala akiwa kule Samaria kwa muda wa miaka makumi mbili. 28 Alitenda maovu mbele ya Yawe; hakuacha zambi za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. 29 Wakati wa utawala wa Peka mufalme wa Israeli, Tigilati-Pileseri, mufalme wa Asuria, aliteka miji ya Iyoni, Abeli-Beti-Maka, Yanoa, Kadesi na Hazori, pamoja na inchi za Gileadi, Galilaya na Nafutali na kuwahamisha wakaaji wake kwenda Asuria. 30 Katika mwaka wa makumi mbili wa utawala wa Yotamu mwana wa Uzia mufalme wa Yuda, Hoshea mwana wa Ela alimwasi Peka mwana wa Remalia na kumwua, kisha akatawala kwa pahali pake. 31 Mambo mengine ya Peka na yote aliyoyafanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. Mufalme Yotamu wa Yuda ( 2 Sik 27.1-9 ) 32 Katika mwaka wa pili wa utawala wa Peka mwana wa Remalia katika inchi ya Israeli, Yotamu mwana wa Uzia, mufalme wa Yuda, akaanza kutawala Yuda. 33 Alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano alipoanza kutawala, akatawala akiwa kule Yerusalema kwa muda wa miaka kumi na sita. Mama yake aliitwa Yerusa, binti ya Zadoki. 34 Yotamu alitenda kwa usawa mbele ya Yawe kama vile baba yake Uzia alivyotenda. 35 Hata hivyo, nafasi za kutambikia miungu ya uongo hazikuharibiwa, na watu waliendelea kutambikia na kufukiza ubani kwenye nafasi za juu. Yotamu alijenga mulango wa kaskazini wa nyumba ya Yawe. 36 Mambo mengine ya Yotamu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. 37 Wakati wa utawala wa Yotamu, Yawe akaanza kutuma mufalme Resini wa Aramu na mufalme Peka wa Israeli kwa kushambulia inchi ya Yuda. 38 Yotamu akakufa na kuzikwa katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi. Mwana wake Ahazi akatawala kwa pahali pake. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo