2 Wafalme 10 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wazao wa Ahabu wanauawa 1 Katika muji wa Samaria kulikuwa wana makumi saba wa Ahabu. Yehu akaandika barua na kutuma barua kwa watawala wa muji, kwa viongozi na kwa walinzi wa wana wa Ahabu. Barua yenyewe ilisema hivi: 2 “Kwa sababu kati yenu kuna wana wa mufalme, vilevile kuna farasi na magari, silaha na miji yenye kuta, 3 muchague na kumuweka mwenye uwezo zaidi kati ya wana wa mufalme kuwa mufalme. Halafu mupigane vita kwa ajili ya ukoo wa mufalme.” 4 Watawala wa Samaria waliogopa sana na kusema: “Tunaweza namna gani kumupiga Yehu wakati mufalme Yoramu na mufalme Ahazia hawakuweza?” 5 Kwa hiyo mukubwa wa nyumba ya mufalme na musimamizi wa muji, wakishirikiana na viongozi wengine na walinzi, wakamupelekea Yehu ujumbe huu: “Sisi ni watumwa wako, na tuko tayari kufanya lolote unalosema. Lakini hatutamuweka mutu yeyote kuwa mufalme. Fanya unavyotaka.” 6 Yehu akawaandikia barua ingine akiwaambia: “Ikiwa kweli muko tayari kufuata maagizo yangu, mulete hapa Yezereheli vichwa vya wana wa bwana wenu nivipate kesho kwa wakati kama huu.” Wana makumi saba wa mufalme Ahabu waliishi kwa viongozi wa Samaria, ambao walikuwa walezi wao. 7 Basi, barua ilipowafikia, waliwatwaa hao wana wa mufalme na kuwakata vichwa wote makumi saba. Waliweka vichwa vyao katika vikapu na kumupelekea Yehu kule Yezereheli. 8 Kisha mutumishi mumoja akamwendea na kusema: “Vichwa vya wana wa mufalme vimekwisha kuletwa.” Halafu akaamuru: “Muviweke chini katika mafungu mawili kwenye mulango wa muji, muviache vikae kule mpaka asubui.” 9 Asubui yake akatoka, akasimama na kuwaambia watu wote: “Ninyi ni watu wa haki. Mimi nilifanya mupango wa kuasi bwana wangu na kumwua. Lakini ni nani aliyewaua hawa wote? 10 Mujue kwamba maneno yote Yawe aliyosema juu ya jamaa ya Ahabu yametimia. Yawe ameyafanya hayo aliyosema kwa njia ya mutumishi wake Elia.” 11 Halafu Yehu akaua jamaa yote ya Ahabu iliyokuwa inakaa Yezereheli, pamoja na wakubwa wake na warafiki na makuhani wake. Hakumwacha hata mutu yeyote. Watu wa jamaa ya Ahazia wanauawa 12 Kisha Yehu aliondoka Yezereheli, akaelekea Samaria. Akiwa katika njia pahali panapoitwa “Kambi ya Wachungaji”, 13 alikutana na watu wa jamaa ya marehemu Ahazia mufalme wa Yuda akawauliza: “Ninyi ni wa nani?” Wakamujibu: “Sisi ni watu wa jamaa ya Ahazia. Tumeteremuka huku kuwatembelea wana wa mufalme na wana wa malkia.” 14 Kisha akaamuru: “Muwakamate wakiwa wazima.” Wakawakamata watu makumi ine na wawili wakawaua karibu na kisima cha “Kambi ya Wachungaji”. Hakuna aliyebaki hata mumoja. 15 Yehu akatoka tena na alipofika katika njia akakutana na Yonadabu mwana wa Rekabu. Yehu akamusalimia, kisha akamwuliza: “Wewe una mawazo sawa na yangu? Utajiunga nami na kunisaidia?” Yonadabu akamujibu: “Ndiyo, nitajiunga nawe.” Yehu akasema: “Basi, unipe mukono wako.” Wakashikana mikono na Yehu akamupandisha ndani ya gari lake. 16 Akamwambia: “Fuatana nami kusudi ujionee jinsi ninavyokuwa mwaminifu kwa Yawe.” Basi, wakasafiri pamoja katika gari lake. 17 Walipofika Samaria, Yehu aliua jamaa yote ya Ahabu bila kumwacha hata mumoja wao, sawa vile Yawe alivyomwambia Elia itakavyokuwa. Wafuasi wa Bali wanauawa 18 Yehu akawakusanya watu wa Samaria na kuwaambia: “Mufalme Ahabu alimutumikia Bali kidogo tu, lakini mimi nitamutumikia zaidi. 19 Uwaite manabii wote wa Bali, wafuasi wake wote na makuhani. Ni sharti kila mumoja afike, maana ninataka kumutolea Bali sadaka kubwa, na yeyote atakayekosa kufika atauawa.” Hiyo ilikuwa ni namna ya Yehu ya kudanganya kusudi apate kuwaua wafuasi wa Bali. 20 Yehu akaamuru: “Mutangaze mukutano wa ibada ya Bali!” Tangazo likatolewa, 21 na Yehu akapeleka habari katika inchi yote ya Israeli kusudi wafuasi wote wa Bali wahuzurie kila mumoja. Wakakuja wote na kujaa katika hekalu la Bali kutoka pembe moja mpaka nyingine. 22 Halafu Yehu akamwagiza yule aliyesimamia nguo za ibada hivi: “Ondoa nguo na kuwapa watu wote wanaotumikia Bali.” Musimamizi akatoa nguo zile, akawapa. 23 Halafu Yehu akaingia katika hekalu la Bali akifuatana na Yonadabu na kuwaambia waliokuwa ndani ya hekalu: “Muhakikishe kwamba wanaokuwa humu ndani ya hekalu ni wale wanaomwabudu Bali tu, na kwamba hakuna mutu yeyote anayemwabudu Yawe.” 24 Kisha akaingia pamoja na Yonadabu kwa kumutolea Bali matoleo na sadaka za kuteketezwa. Yehu alikuwa ameweka watu makumi tatu inje ya hekalu na kuwapa maagizo haya: “Muwaue watu hawa wote. Yeyote atakayemwacha hata mumoja wao atoroke atalipa kwa maisha yake!” 25 Mara tu Yehu alipomaliza kutoa sadaka ya kuteketezwa, aliwaambia walinzi na wakubwa: “Muingie muwaue wote. Musimwache hata mumoja atoroke!” Wakaingia na panga zao tayari na kuwaua wote, kisha wakatoa maiti zao inje. Halafu wakaingia katika chumba cha ndani cha hekalu, 26 na kutoa nguzo takatifu na kuiteketeza kwa moto. 27 Wakaharibu nguzo pamoja na hekalu; wakaigeuza hekalu kuwa choo, na hivi ndivyo inavyokuwa mpaka hivi leo. 28 Hivi ndivyo Yehu alivyomaliza ibada za Bali katika Israeli. 29 Lakini hakuacha zambi zile za Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma Waisraeli watende zambi, ni kusema ile ibada ya sanamu za wana-ngombe wa zahabu kule Beteli na Dani. 30 Yawe akamwambia Yehu: “Umewatendea wazao wa Ahabu yale yote niliyotaka uwatendee. Kwa hiyo nimekuahidi kwamba wazao wako mpaka kizazi cha ine watatawala Israeli.” 31 Lakini Yehu hakutii sheria za Yawe, Mungu wa Israeli, kwa moyo wake wote. Hakuacha zambi zile za Yeroboamu ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. Kifo cha Yehu 32 Wakati ule Yawe alianza kupunguza eneo la inchi ya Israeli. Mufalme Hazaeli wa Aramu akashinda inchi yote ya Israeli 33 katika upande wa mashariki ya muto Yordani, na inchi za Gileadi, Gadi, Rubeni na Manase na kutoka muji wa Aroeri unaokuwa kwenye bonde la Arnoni, kwenye inchi za Gileadi na Basani. 34 Mambo mengine ya Yehu, yote aliyofanya na ushujaa wake yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. 35 Akakufa na kuzikwa Samaria. Mwana wake Yoahazi akatawala kwa pahali pake. 36 Yehu alitawala Israeli akiwa Samaria kwa miaka makumi mbili na minane. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo