2 Wafalme 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Elia na mufalme Ahazia 1 Kisha kufa kwa Ahabu, watu wa Moabu waliasi wasitawaliwe na Israeli. 2 Mufalme Ahazia alipokuwa Samaria alianguka kutoka chumba kilichokuwa juu ya paa ya nyumba yake, akaumia vibaya. Kwa hiyo akawatuma wajumbe, akawaambia: “Muende kwa Bali-Zebubu, mungu wa muji wa Ekuroni, mumwulize kama nitapona ugonjwa huu.” 3 Lakini malaika wa Yawe akamwambia nabii Elia wa muji wa Tisibe, aende kukutana na wajumbe hao na kuwauliza: “Kwa nini munakwenda kwa Bali-Zebubu, mungu wa Ekuroni? Hakuna Mungu katika inchi ya Israeli? 4 Mumwambie mufalme kwamba Yawe amesema hivi: ‘Hautashuka katika kitanda ulichopanda juu yake. Hakika utakufa.’ ” 5 Basi, Elia akawaendea. Wale wajumbe wakarudi kwa mufalme, naye akawauliza: “Mbona mumerudia?” 6 Wakamujibu: “Tumekutana na mutu ambaye alitutuma turudi kukuambia kwamba Yawe amesema hivi: ‘Kwa nini unatuma wajumbe kwa Bali-Zebubu, mungu wa Ekuroni? Hakuna Mungu katika inchi ya Israeli? Hautashuka katika kitanda ulichopanda juu yake. Hakika utakufa.’ ” 7 Mufalme akauliza: “Ni mutu gani yule aliyekutana nanyi na kuwaambia mambo hayo?” 8 Wao wakamujibu: “Alikuwa akivaa nguo ya manyoya na mukaba wa ngozi kwenye kiuno.” Mufalme akasema: “Yule ni Elia wa Tisibe!” 9 Halafu akamutuma kiongozi mumoja wa waaskari na watu wake makumi tano wamulete Elia. Kiongozi huyo akaenda, akamukuta Elia akiikaa kwenye mulima, akamwambia: “Ewe mutu wa Mungu, mufalme anakuamuru ushuke.” 10 Elia akamujibu yule kiongozi wa watu makumi tano: “Kama kweli mimi ni mutu wa Mungu, moto ushuke kutoka mbinguni na kukuteketeza wewe pamoja na watu wako!” Mara moja moto ukashuka kutoka mbinguni, ukamuteketeza pamoja na watu wake makumi tano. 11 Mufalme akamutuma kiongozi mwingine na watu wake makumi tano wamulete Elia. Naye akamwambia Elia: “Ewe mutu wa Mungu, mufalme anakuamuru ushuke mara moja!” 12 Elia akamujibu: “Kama kweli mimi ni mutu wa Mungu, moto ushuke kutoka mbinguni na kukuteketeza wewe pamoja na watu wako!” Mara moja moto wa Mungu ukashuka kutoka mbinguni, ukamuteketeza pamoja na watu wake makumi tano. 13 Kwa mara ingine tena, mufalme akatuma kiongozi mwingine na watu wake makumi tano. Kiongozi wa tatu akapanda kwenye mulima, akapiga magoti mbele ya Elia na kumusihi akisema: “Ewe mutu wa Mungu, ninakusihi uyahesabu maisha yangu na maisha ya hawa watumishi wako makumi tano yakuwe ya bei kali mbele yako. 14 Viongozi wawili waliotangulia na watu wao, wameteketezwa na moto ulioshuka toka mbinguni; lakini sasa ninakuomba uhurumie maisha yangu.” 15 Malaika wa Yawe akamwambia Elia: “Shuka pamoja naye, wala usimwogope.” Basi, Elia akasimama, akashuka pamoja naye mpaka kwa mufalme. 16 Akamwambia mufalme: “Yawe anasema hivi: ‘Kwa sababu ulituma wajumbe kuomba shauri kwa Bali-Zabubu mungu wa Ekuroni sawa vile hakuna Mungu katika Israeli ambaye ungemwomba shauri, basi, hautashuka katika kitanda ambacho umepanda juu yake. Hakika utakufa.’ ” 17 Kisha Ahazia akakufa kama vile Yawe alivyomwambia nabii wake Elia. Na kwa sababu Ahazia hakukuwa na mutoto mwanaume, Yoramu akakuwa mufalme kwa pahali pake, katika mwaka wa pili wa utawala wa Yehoramu mwana wa Yosafati, mufalme wa Yuda. 18 Mambo mengine mufalme Ahazi aliyoyatenda yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo