2 Timoteo 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Ninakuamuru mbele ya Mungu na mbele ya Kristo Yesu atakayewahukumu wazima na wafu na kufuatana na kurudi kwake kwa kutawala: 2 utangaze Neno la Mungu kwa nguvu kwa wakati unaofaa na kwa wakati usiofaa. Ukaripe, usahihishe na kuonya ukifundisha kwa uvumilivu. 3 Maana kutakuja wakati watu watakapokataa kusikiliza mafundisho ya kweli, lakini watafuata tamaa zao wenyewe wakijitafutia walimu wengi kwa kuwafundisha mambo yale wanayotamani kusikia. 4 Watafunga masikio yao wasisikilize mambo ya kweli na kusikiliza hadisi za uongo. 5 Lakini wewe, ujiangalie katika mambo yote, uvumilie mateso, ufanye kazi yako ya kuhubiri Habari Njema na kutimiza kabisa utumishi wako. 6 Kwa maana, mimi sasa niko tayari kutolewa kama sadaka, na wakati wa kufa kwangu umekaribia. 7 Nimeshindana vizuri, nimekimbia na kufika mwisho wa mashindano yangu. Nimelinda imani yangu. 8 Tangia sasa nimetayarishiwa zawadi ya ushindi, ndiyo ile taji ya haki, ambayo Bwana anayekuwa Mwamuzi wa haki atakayonipa siku ile ya kurudi kwake. Wala hatanipa mimi peke yangu tu, lakini na wale wote wanaopenda kumwona wakati atakaporudi. Maagizo mbalimbali ya pekee 9 Ufanye nguvu kufika kwangu upesi. 10 Dema amependelea mambo ya dunia hii akaniacha na kwenda Tesalonika. Kreske akaenda Galatia, na Tito akaenda Dalmatia. 11 Luka peke yake ndiye anayekuwa hapa pamoja nami. Umutwae Marko, ukuje pamoja naye, kwa sababu ananifalia katika kazi yangu. 12 Nimemutuma Tikiko kule Efeso. 13 Wakati utakapokuja uniletee koti niliyoacha kule Troa kwa Karpo; uniletee vilevile vitabu, hasa vile vya ngozi. 14 Alesanduro, yule mufua vyuma amenitendea mabaya mengi. Bwana atamulipa kufuatana na matendo yake. 15 Nawe vilevile ujilinde naye kwa sababu alipinga kwa nguvu maneno yetu yote. 16 Nilipojitetea kwa mara ya kwanza hakuna hata mutu mumoja aliyenisaidia; wote waliniachilia. Mungu asiwahesabie makosa yao! 17 Lakini Bwana alinisaidia, akanitia nguvu nipate kuitangaza Habari Njema kwa ukamilifu kusudi watu wa mataifa mengine wapate kuisikia. Nami nikaokolewa toka katika kinywa cha simba. 18 Bwana ataniokoa toka katika mambo yote mabaya na kunipeleka salama katika Ufalme wake wa mbinguni. Bwana atukuzwe milele na milele. Amina. Salamu 19 Unisalimie Prisila na Akila na jamaa la Onesiforo vilevile. 20 Erasto alibakia Korinto, na nilimwacha Trofimo kule Mileto kwa sababu alikuwa mugonjwa. 21 Ufanye nguvu kufika mbele ya wakati wa baridi kali. Eubulo, Pude, Lino, Klaudia na wandugu wote waamini wanakusalimia. 22 Bwana akulinde. Ninawatakia neema kutoka kwa Mungu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo