Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

2 Timoteo 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Maonyo ya siku za mwisho

1 Ujue vizuri kwamba siku za mwisho zitakuwa nyakati za magumu.

2 Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda feza, wenye kujisifu na wenye kiburi, wenye kukufuru, wasiotii wazazi wao, wasioshukuru na waovu.

3 Hawatakuwa na upendo wala huruma. Watakuwa wenye kusingiziana, wasiojizuiza, wakali na wasiopenda mema.

4 Watakuwa wenye kutoana, wenye kichwa kigumu, wenye majivuno na wenye kupenda tamaa ya vitu kuliko kumupenda Mungu.

5 Kwa inje watajionyesha kama watu wenye kushikamana na ibada, lakini wanazarau uwezo wake. Ujiepushe na watu hao.

6 Kwa maana kati yao kuna wamoja wanaojiingiza katika nyumba za watu na kuwashawishi wanawake wajinga wanaolemewa na mizigo ya zambi na kuvutwa na tamaa za namna nyingi.

7 Wanawake wale wanataka kujifunza siku zote, lakini hawafikii kutambua ukweli.

8 Watu wale wanapinga ukweli kama vile Yane na Yambure walivyopingana na Musa. Akili ya watu hao imepotoka, nayo imani yao imegeuka bure.

9 Lakini hawataendelea mbali sana, kwa sababu upumbafu wao utaonekana wazi mbele ya watu wote, sawa ilivyokuwa kwa Yane na Yambure.


Maagizo ya mwisho

10 Lakini wewe umefuata kabisa mufano wangu katika mafundisho yangu na mwenendo wangu, makusudi yangu, imani yangu, uvumilivu wangu, upendo wangu, ungojevu wangu,

11 mateso na taabu yangu. Unajua mambo yote ambayo yalinitokea kule Antiokia, Ikonio na Listra. Mateso haya niliyavumilia, na Bwana akaniokoa katika yote.

12 Nao wote wanaotaka kuishi maisha ya kumwabudu Mungu katika kuungana na Kristo Yesu, watateswa.

13 Lakini watu waovu na wadanganyifu wataendelea katika maovu, wakipotosha watu wengine na kujipotosha wenyewe.

14 Lakini wewe ushikamane na mambo yale uliyofundishwa na kuyaamini kabisa. Unajua ni nani aliyekufundisha.

15 Tena, tangia utoto wako unajua Maandiko Matakatifu yanayoweza kukupatia hekima kusudi uokolewe kwa njia ya kumwamini Kristo Yesu.

16 Maandiko yote Matakatifu yameandikwa kwa maongozi ya Mungu na yanafaa kwa kufundisha, kuonya, kuhakikisha na kuadibisha katika haki,

17 kusudi mutu wa Mungu apate kukamilika na kuwa tayari kabisa kwa kutenda kila kazi njema.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan