2 Samweli 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Daudi anafanywa kuwa mufalme wa Yuda 1 Nyuma ya mambo yale, Daudi alimwomba Yawe shauri, akasema: “Niende kwenye muji mumoja kati ya miji ya Yuda?” Yawe akamwambia: “Kwenda!” Daudi akamwuliza: “Niende katika muji gani?” Yawe akamujibu: “Kwenda kwenye muji wa Hebroni.” 2 Kwa hiyo Daudi alikwenda Hebroni, pamoja na wake zake wawili, Ahinoamu wa Yezereheli, na Abigaili, mujane wa Nabali, kutoka muji wa Karmeli. 3 Aliwapeleka watu wake, kila mutu akiwa pamoja na jamaa yake; nao wakafanya makao yao katika miji iliyokuwa kandokando ya Hebroni. 4 Watu wa Yuda walimwendea Daudi kule Hebroni wakamupakaa mafuta akuwe mufalme wao. Daudi aliposikia kwamba watu wa Yabesi-Gileadi ndio waliomuzika Saulo, 5 aliwatuma watu kule Yabesi-Gileadi na ujumbe: “Yawe awabariki kwa maana mulitendea bwana wenu Saulo mema kwa kumuzika. 6 Sasa, Yawe awatendee kwa wema na uaminifu. Nami nitawatendea vizuri kutokana na jambo mulilolitenda. 7 Lakini mukuwe imara na mashujaa. Saulo, bwana wenu, amekufa, na watu wa Yuda wamenipakaa mafuta nikuwe mufalme wao.” Isiboseti anafanywa kuwa mufalme wa Israeli 8 Abeneri mwana wa Neri, mukubwa wa waaskari wa Saulo alikuwa amemukamata Isiboseti mwana wa Saulo na kumupeleka kule Mahanaimu. 9 Kule, Abeneri akamusimika Isiboseti kuwa mufalme wa inchi ya Gileadi, Asheri, Yezereheli, Efuraimu na Benjamina na Israeli yote. 10 Isiboseti alikuwa na umri wa miaka makumi ine alipoanza kuitawala Israeli, naye alitawala kwa muda wa miaka miwili. Lakini kabila la Yuda lilimufuata Daudi. 11 Daudi alikuwa mufalme wa kabila la Yuda kwa muda wa miaka saba na nusu, makao yake yalikuwa kule Hebroni. Vita kati ya watu wa Israeli na watu wa Yuda 12 Abeneri mwana wa Neri, pamoja na watumishi wa Isiboseti mwana wa Saulo, waliondoka Mahanaimu na kwenda Gibeoni. 13 Yoabu mwana wa Zeruya na watumishi wengine wa Daudi, nao walitoka na kukutana na Abeneri na watu aliokuwa nao kwenye kiziwa kinachokuwa kule Gibeoni. Kikundi kimoja kikajipanga upande mumoja wa kiziwa na kingine upande mwingine. 14 Abeneri akamwambia Yoabu: “Uwaruhusu vijana wapigane mbele yetu!” Yoabu akamujibu: “Sawa.” 15 Halafu vijana makumi mbili na ine wakatolewa: upande wa kabila la Benjamina na Isiboseti mwana wa Saulo, vijana kumi na wawili; na upande wa Daudi, vijana kumi na wawili. 16 Kila mumoja alimukamata adui yake kwenye kichwa, na kumuchoma upanga katika ubavu. Hivyo wote wawili wakaanguka chini, wamekufa. Kwa hiyo, pahali pale pakaitwa Shamba la Mapanga. Pahali pale pako kule Gibeoni. 17 Vita ya siku hiyo ilikuwa kali. Abeneri na watu wa Israeli walipigwa vibaya na watu wa Daudi. 18 Wana watatu wa Zeruya, Yoabu, Abisayi na Asaeli walikuwa pale pale. Asaeli alikuwa na mbio kama paa. 19 Asaeli alimufuatilia Abeneri moja kwa moja bila kugeuka upande wa kuume wala kushoto. 20 Abeneri alipoangalia nyuma na kumwona Asaeli, alimwambia: “Ni wewe Asaeli?” Yeye akamujibu: “Kweli, ni mimi.” 21 Abeneri akamwambia: “Geukia upande wa kuume au kushoto, umukamate kijana mumoja na kutwaa vitu vyake.” Lakini Asaeli hakuacha kumufuatilia. 22 Abeneri akamwambia Asaeli mara ya pili: “Acha kunifuatilia. Kwa nini nikuue? Nitaweza kuonana na kaka yako Yoabu?” 23 Lakini Asaeli alikataa. Kwa hiyo Abeneri akamupiga mukuki ndani ya tumbo kinyumenyume, na mukuki huo ukatokea katika mugongo wa Asaeli. Asaeli akaanguka chini na kufa pale pale. Watu wote waliofika pahali Asaeli alipokufia, walisimama kimya. 24 Lakini Yoabu na Abisayi walimufuatilia Abeneri. Jua lilipokuwa linatua wakafika kwenye mulima Ama, unaokuwa upande wa mashariki ya Gia, katika barabara inayokwenda katika jangwa la Gibeoni. 25 Watu wa kabila la Benjamina wakajikusanya pamoja, wakakuwa nyuma ya Abeneri, hivyo wakaunda kikundi chao, nao wakasimama juu ya mulima. 26 Kisha Abeneri akamwita Yoabu: “Tutapigana siku zote? Hauoni kwamba mwisho utakuwa muchungu? Utaendelea kwa muda gani bila kuwashawishi watu wako kuacha kuwafuatilia wandugu zao?” 27 Yoabu akamwambia: “Kama vile Yawe anavyoishi, ungekuwa haujasema jambo lile, hakika watu wangu wangeendelea kuwafuatilia wandugu zao mpaka kesho asubui.” 28 Kwa hiyo, Yoabu akapiga baragumu na watu wakaacha kuwafuatilia watu wa Israeli, wala hawakupigana zaidi. 29 Abeneri na watu wake walipita katika bonde la Araba usiku kucha. Wakavuka Yordani, wakatembea muchana wote mpaka Mahanaimu. 30 Yoabu aliporudi kutoka kumufuatilia Abeneri, aliwakusanya watu wake wote, akagundua kwamba watumishi kumi na tisa wa Daudi walikosekana, bila kuhesabu Asaeli. 31 Lakini watumishi wa Daudi walikuwa wamewaua watu mia tatu makumi sita kutoka kabila la Benjamina pamoja na watu wa Abeneri. 32 Yoabu na watu wake walipeleka mwili wa Asaeli, wakauzika kwenye kaburi la baba yake, linalokuwa kule Betelehemu. Yoabu na watu wake walitembea usiku kucha, na kulipokucha wakafika katika muji wa Hebroni. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo