2 Samweli 19 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yoabu anamukaripia mufalme 1 Hapo mufalme alishikwa na huzuni kubwa, akapanda kwenye chumba kilichokuwa juu ya mulango na kulia. Alipokuwa anapanda, alilia akisema: “Mwana wangu Abusaloma, mwana wangu Abusaloma! Ingekuwa heri ningalikufa pahali pako! Ole, Abusaloma mwana wangu! Mwana wangu!” 2 Yoabu alipata habari kwamba mufalme alikuwa akilia na kuomboleza juu ya kifo cha Abusaloma. 3 Ushindi wa siku hiyo uligeuzwa kuwa maombolezo kwa watu wote, waliposikia kwamba mufalme anamwombolezea Abusaloma. 4 Kwa hiyo, siku hiyo, watu waliingia katika muji kimyakimya kama watu wanaorudi katika muji wakipata haya kwa kukimbia vita. 5 Mufalme alijifunika uso wake na kulia kwa sauti kubwa akisema: “Ole mwana wangu Abusaloma! Ole, Abusaloma, mwana wangu! Mwana wangu!” 6 Halafu Yoabu aliingia katika nyumba ya mufalme, akamwambia: “Leo umetupatisha haya sisi watumishi wako wote ambao leo tumeyaokoa maisha yako, maisha ya watoto wako wanaume, na maisha ya watoto wako wanawake, maisha ya wake zako na maisha ya wahabara zako. 7 Wewe unawapenda wale wanaokuchukia na unawachukia wale wanaokupenda. Umetuonyesha waziwazi leo kwamba majemadari na watumishi wako hawana maana kwako. Ninaona leo, kama Abusaloma angekuwa muzima, na sisi wote tungalikufa, ungeona ni sawa. 8 Sasa, simama uzungumuze na watumishi wako kwa upole. Maana, ninaapa kwa Yawe, kama hauendi kuzungumuza nao, hakuna hata mumoja atakayebaki pamoja nawe leo magaribi. Hili litakuwa jambo baya zaidi kwako kuliko maovu yote yaliyokupata tangu ujana wako mpaka leo.” 9 Kisha, mufalme akatoka, akaenda, akaikaa kwenye nafasi yake karibu na mulango. Watu wote walipoambiwa kwamba mufalme yuko kwenye mulango, wote walimwendea. Wakati ule, watu wote wa Israeli walikuwa wamekimbia, kila mumoja kwake. Daudi anajitayarisha kurudi Yerusalema 10 Watu wote walikuwa wanabishana wao kwa wao katika makabila yote ya Israeli, wakisema: “Mufalme Daudi alitukomboa toka mikono ya waadui zetu, alituokoa toka mikono ya Wafilistini. Lakini sasa ameikimbia inchi, akimukimbia Abusaloma. 11 Tena Abusaloma ambaye tulimupakaa mafuta akuwe mufalme wetu, sasa ameuawa katika vita. Sasa, kwa nini hatuzungumuzii juu ya kumurudisha mufalme Daudi?” 12 Mufalme Daudi akatuma ujumbe kwa makuhani Zadoki na Abiatari: “Muwaambie wazee wa Yuda: ‘Kwa nini ninyi ndio mutakuwa wa mwisho kumurudisha mufalme katika nyumba yake? Maneno yote Waisraeli waliyosema yamenifikia mimi mufalme. 13 Ninyi ni wandugu zangu, ninyi ni damu yangu. Kwa nini mukuwe wa mwisho kunirudisha mimi mufalme kwangu? 14 Muulize vilevile Amasa kama yeye si damu yangu. Tena Mungu aniue ikiwa simufanyi yeye kuwa jemadari wa kundi langu la waaskari tangu leo pahali pa Yoabu.’ ” 15 Kwa hiyo, Daudi aliivuta mioyo ya watu wote wa Yuda kama mutu mumoja. Halafu, wakamupelekea ujumbe kusema: “Rudi kwako, wewe na watumishi wako wote.” 16 Basi, mufalme akakuja kwenye muto Yordani na watu wote wa Yuda wakakuja mpaka Gilgali kwa kumupokea mufalme na kumuvukisha muto Yordani. Daudi anamusamehe Simei 17 Simei mwana wa Gera, wa kabila la Benjamina, kutoka Bahurimu, alifanya haraka kwenda pamoja na watu wengine kwa kumupokea mufalme Daudi. 18 Simei alikwenda pamoja na watu wa kabila la Benjamina elfu moja. Siba mutumishi wa jamaa ya Saulo, pamoja na watoto wake kumi na watumishi makumi mbili, walikwenda haraka kwenye muto Yordani kumutangulia mufalme Daudi. 19 Basi, wakavuka kwenye kivuko kwa kuisindikiza jamaa ya mufalme na kumufanyia mufalme yote aliyoyapenda. Simei mwana wa Gera akakuja, akajitupa mbele ya mufalme, akainama uso mpaka chini, wakati mufalme alipokuwa karibu kuvuka muto Yordani. 20 Simei akamwambia mufalme: “Ninakuomba, bwana wangu mufalme, usinihesabu kuwa na kosa wala kukumbuka kosa nililofanya siku ile ulipokuwa ukiondoka Yerusalema. Ninakuomba usiyaweke hayo ndani ya moyo. 21 Maana, mimi mutumishi wako ninajua kwamba nilitenda zambi. Hii ndiyo sababu nimekuja leo, nikiwa wa kwanza katika kabila la Yosefu kuja kukupokea wewe bwana wangu, mufalme.” 22 Halafu Abisayi mwana wa Zeruya akasema: “Si Simei anapaswa kuuawa maana alimulaani muchaguliwa wa Yawe?” 23 Lakini Daudi akasema: “Wana wa Zeruya, kuna maneno gani kati yangu nanyi. Kwa nini munajifanya kama waadui zangu leo? Basi inawezekana kwa mutu yeyote katika Israeli kuuawa kwa siku ya leo? Sijui kwamba mimi ni mufalme wa Israeli siku ya leo?” 24 Kisha, mufalme akamwambia Simei: “Wewe hautauawa.” Mufalme akamwapia Simei. Daudi anamusamehe Mefiboseti 25 Mefiboseti mujukuu wa Saulo alikwenda vilevile kumupokea mufalme Daudi. Tangu siku ile mufalme alipoondoka Yerusalema mpaka wakati aliporudi salama, Mefiboseti alikuwa hajapata kunawa miguu yake, kukata ndevu zake wala hakujali kufua nguo zake. 26 Basi, alipofika Yerusalema kwa kumupokea mufalme, Daudi alimwuliza: “Mefiboseti, kwa nini haukuandamana pamoja nami?” 27 Mefiboseti akasema: “Ee bwana wangu mufalme, mutumishi wangu alinidanganya. Maana, mimi mutumishi wako, nilimwambia: ‘Unitandikie punda nipate kupanda juu yake kwenda pamoja na mufalme’, maana mimi mutumishi wako ni kilema. 28 Sasa, amenisingizia kwako, ee bwana wangu mufalme. Lakini wewe, bwana wangu mufalme, uko kama malaika wa Mungu. Fanya sawa unavyotaka. 29 Maana, jamaa yote ya babu yangu walikuwa watu ambao wamestahili kuuawa mbele yako, bwana wangu mufalme. Lakini uliniweka mimi mutumishi wako kati ya wale wanaokula kwenye meza yako. Nina haki yoyote zaidi hata nikulilie mufalme?” 30 Mufalme akamwambia: “Usiniambie zaidi juu ya mambo yako pekee. Mimi nimekwisha amua kuwa wewe pamoja na Siba mutagawanyana inchi ya Saulo.” 31 Lakini Mefiboseti akamwambia mufalme: “Umuruhusu Siba atwae inchi yote peke yake. Mimi nimetosheka kwamba wewe bwana wangu mufalme umerudi kwako salama.” Daudi anamutendea Barzilayi wema 32 Barzilayi wa Gileadi alikuwa amefika kutoka Rogelimu. Alikuwa amekwenda pamoja na mufalme kwenye muto Yordani kwa kumusindikiza mpaka ngambo ya muto. 33 Barzilayi alikuwa muzee sana, mwenye umri wa miaka makumi nane. Naye Barzilayi alikuwa amemutunza mufalme alipokaa kule Mahanaimu, kwa sababu alikuwa tajiri sana. 34 Basi, mufalme Daudi akamwambia Barzilayi: “Twende wote kule Yerusalema nami nitakutunza.” 35 Lakini Barzilayi akamwambia mufalme: “Niko tena na miaka mingi ya kuishi ndipo niende nawe mufalme mpaka Yerusalema? 36 Mimi leo nina umri wa miaka makumi nane. Niko na uwezo wa kutambua yanayokuwa mazuri na yale yasiyokuwa mazuri? Mimi mutumishi wako ninaweza tena kutambua onjo ya kile ninachokula au kunywa? Nitaweza tena kutambua uzuri wa sauti za waimbaji wanaume au wanawake? Kwa nini mimi mutumishi wako nikuwe muzigo wa zaidi kwako bwana wangu mufalme? 37 Mimi mutumishi wako nitakwenda nawe mwendo mufupi ngambo ya Yordani. Kwa nini, mufalme anilipe zawadi kubwa hivyo? 38 Ninakuomba uniruhusu mimi mutumishi wako, nikufie katika muji wangu, karibu na kaburi la baba yangu na mama yangu. Lakini huyu mutumishi wako Kimuhamu, umuruhusu aende pamoja nawe bwana wangu mufalme, na umutendee yeye lolote unaloona ni zuri.” 39 Mufalme akamwambia: “Kimuhamu atakwenda nami, na nitamutendea lolote unaloona ni zuri. Na lolote utakalotaka nikutendee, nitakutendea.” 40 Halafu watu wote wakavuka muto Yordani na mufalme naye akavuka. Mufalme akamubusu na kumubariki Barzilayi, na Barzilayi akarudi kwake. Watu wa Yuda na watu wa Israeli wanabishana juu ya mufalme 41 Mufalme aliendelea mpaka Gileadi. Kimuhamu akakuwa anafuatana naye. Watu wote wa Yuda na nusu ya watu wa Israeli walikuwa wakimusindikiza mufalme. 42 Kisha, watu wote wa Israeli wakakuja kwa mufalme na kumwambia: “Kwa nini wandugu zetu watu wa Yuda walikuwa wamekutwaa ukiwa katika njia, wakakuvukisha muto Yordani, wewe na jamaa yako, pamoja na watu wako?” 43 Watu wa Yuda wakawaambia watu wa Israeli: “Kwa sababu mufalme ni ndugu yetu wa karibu. Kwa nini munakasirika juu ya jambo hili? Tumekula nini wakati wowote kutoka kwake? Au yeye ametupatia zawadi yoyote?” 44 Watu wa Israeli wakawajibu watu wa Yuda: “Tuna haki mara kumi juu ya mufalme, kuliko zile munazokuwa nazo ninyi, na hata juu ya Daudi mwenyewe. Kwa nini, basi, mulituzarau? Sisi hatukukuwa wa kwanza kusema kwamba mufalme wetu arudishwe?” Maneno ya watu wa Yuda yalikuwa makali kuliko maneno ya watu wa Israeli. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo