2 Samweli 17 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Husayi anamupotosha Abusaloma 1 Zaidi ya hayo, Ahitofeli alimwambia Abusaloma: “Uniruhusu nichague watu elfu kumi na mbili, niondoke na kumufuatia Daudi leo usiku. 2 Nitamushambulia akiwa amechoka na amevunjika moyo, nami nitamutia hofu kubwa. Watu wote wanaokuwa pamoja naye watakimbia. Nitamwua mufalme peke yake, 3 na kuwarudisha watu wengine wote kwako kama bibi arusi anavyorudi katika nyumba ya mume wake. Wewe unayatafuta maisha ya mutu mumoja tu na watu wengine watakuwa na amani.” 4 Shauri hilo la Ahitofeli lilimupendeza Abusaloma na wazee wote wa Israeli. 5 Kisha, Abusaloma akasema: “Mumwite Husayi vilevile, yule mutu wa inchi ya Arki, tusikie neno analotaka kusema.” 6 Husayi alipofika kwa Abusaloma, Abusaloma alimwuliza: “Hivyo ndivyo Ahitofeli alivyosema. Tufanye kama vile alivyotushauria? Kama sivyo, basi, utuambie shauri lako.” 7 Husayi akamwambia Abusaloma: “Wakati huu, shauri Ahitofeli alilolitoa si jema.” 8 Zaidi ya hayo, Husayi akamwambia: “Wewe unajua kwamba baba yako na watu wake ni mashujaa na kwamba wamekasirikishwa kama dubu dike aliyenyanganywa watoto wake katika mbuga. Zaidi ya hayo, unajua kwamba baba yako ni bingwa wa vita. Yeye hatakaa usiku kucha pamoja na watu wake. 9 Hata sasa amekwisha kujificha katika pango moja au nafasi ingine. Ikiwa tu katika mashambulizi ya mwanzo kunakufa watu kati yetu, habari itasambaa kwamba wafuasi wa Abusaloma wameshindwa vibaya. 10 Watu wako watakaposikia hivyo, hata wale ambao ni hodari, wenye mioyo kama ya simba, watavunjika kabisa moyo kwa woga. Maana, Waisraeli wote wanajua kwamba baba yako ni shujaa na wote wanaokuwa pamoja naye ni watu hodari. 11 Shauri langu ni kwamba uwakusanye kwako watu wote wa Israeli tangia Dani mpaka Beri-Seba wakuwe wengi kama muchanga wa bahari, na wewe mwenyewe peke yako uende kwa vita. 12 Nasi tutamwendea Daudi pahali popote anapoweza kupatikana na tutamwangukia sawa vile umande unavyoanguka juu ya udongo. Basi, hakuna atakayebakia hata kama ni yeye mwenyewe au watu wake wote wanaokuwa pamoja naye. 13 Ikiwa atakimbilia katika muji fulani, basi, watu wote wa Israeli wataleta kamba na kukokotea mawe ya majengo yake mpaka katika bonde, na hakutabaki kitu chochote hata jiwe dogo la muji ule.” 14 Abusaloma pamoja na watu wote wa Israeli wakasema: “Shauri la Husayi ni bora kuliko shauri la Ahitofeli.” Wakakataa shauri la Ahitofeli kwa sababu Yawe alikuwa amepanga kulishinda shauri jema la Ahitofeli kusudi aweze kumuletea Abusaloma hasara. Daudi anaonywa na kutoroka 15 Kisha Husayi akawaambia makuhani Zadoki na Abiatari jinsi Ahitofeli na yeye mwenyewe walivyomushauria Abusaloma na wazee wa Israeli. 16 Kisha akasema, “Mupelekee Daudi habari upesi kwamba asilale usiku kwenye vivuko katika jangwa, lakini lazima avuke muto Yordani kusudi asikamatwe na kuuawa, yeye pamoja na watu wake wote.” 17 Wakati ule, Yonatani na Ahimasi walikuwa wakimungojea karibu na Eni-Rogeli, kusudi wasionekane na mutu yeyote wakiingia katika muji. Kila mara mujakazi fulani alikuwa akiwapelekea habari nao wakaipeleka kwa mufalme Daudi. 18 Lakini wakati huu, walionekana na kijana mumoja ambaye alikwenda na kumupasha Abusaloma habari. Kwa hiyo, Yonatani na Ahimasi waliondoka haraka, wakaenda Bahurimu katika nyumba ya mutu fulani aliyekuwa na kisima katika kiwanja chake. Wakaingia ndani ya kisima na kujificha. 19 Mwanamuke mwenye nyumba hiyo akatwaa kifuniko na kukifunika kisima hicho, halafu akaanika ngano juu ya kifuniko. Habari hizo hazikujulikana. 20 Watumishi wa Abusaloma walipofika kwa yule mwanamuke, wakamwambia: “Ahimasi na Yonatani wako wapi?” Yule mwanamuke akawaambia: “Wamekwenda ngambo ya kijito.” Walipowatafuta na kuwakosa, wakarudi Yerusalema. 21 Nyuma ya watumishi wa Abusaloma kuondoka, Yonatani na Ahimasi walitoka ndani ya kisima, wakaenda kwa mufalme Daudi na kumupasha habari. Wakamwambia: “Ondoka, uende ngambo ya muto, kwa sababu Ahitofeli amemushauria Abusaloma juu yako.” 22 Kwa hiyo, Daudi akaondoka na watu wote waliokuwa pamoja naye, wakavuka muto Yordani. Ilipofika asubui hakuna mutu aliyebaki nyuma bila kuvuka muto Yordani. Ahitofeli anajitundika 23 Ahitofeli alipoona kwamba shauri lake halikufuatwa, alitandika punda wake, akaenda kwake, kwenye muji wake. Alipofika kule, alipanga vizuri mambo ya nyumba yake, akajitundika. Akakufa na kuzikwa kwenye kaburi la baba yake. 24 Basi, Daudi akaenda Mahanaimu. Abusaloma akavuka muto Yordani na watu wote wa Israeli. 25 Wakati ule, Abusaloma alikuwa amemuweka Amasa kuwa jemadari wa waaskari pahali pa Yoabu. Amasa alikuwa mwana wa Itira, Mwisimaeli. Mama yake aliitwa Abigaili binti wa Nahasi, aliyekuwa dada ya Zeruya mama ya Yoabu. 26 Abusaloma pamoja na watu wa Israeli walipiga kambi yao katika inchi ya Gileadi. 27-29 Daudi alipofika Mahanaimu, alikutwa na Sobi mwana wa Nahasi wa muji wa Raba katika inchi ya Amoni, Makiri mwana wa Amieli wa muji wa Lodebari, pamoja na Barzilayi wa muji wa Rogelimu katika inchi ya Gileadi. Hawa watu waliona kwamba Daudi na watu wake walikuwa na njaa, walikuwa wanachoka na walikuwa na kiu kwa sababu ya kusafiri katika jangwa. Basi, waliwapelekea vitanda, mabeseni, vyombo vya udongo, ngano, shayiri, unga, mihindi yenye kukaangwa, kunde na manjegere, asali, siagi, kondoo na maziwa kutoka nyama wao wa kufugwa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo