2 Samweli 14 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yoabu anapanga kumurudisha Abusaloma 1 Yoabu mwana wa Zeruya alitambua kwamba moyo wa Daudi ulikuwa unamwelekea Abusaloma tu. 2 Kwa hiyo alituma watu kule Tekoa kusudi wamutafutie mwanamuke mwenye hekima. Walipomuleta, akamwambia: “Ujifanye sawa vile mwenye kuwa na kilio. Vaa nguo za kilio, usijipakae mafuta, lakini ujifanye kama mwanamuke ambaye amekuwa katika kilio kwa muda murefu. 3 Halafu uende kwa mufalme umwambie yale ninayokuambia.” Kisha Yoabu akamwambia maneno ya kumwambia mufalme. 4 Huyo mwanamuke kutoka Tekoa akaenda kwa mufalme, akainama uso mpaka chini mbele ya mufalme, akamwambia: “Ee mufalme, unisaidie.” 5 Mufalme akamwambia: “Una shida gani?” Yule mwanamuke akajibu: “Ninasikitika, mimi ni mujane, mume wangu amekufa. 6 Nilikuwa na watoto wanaume wawili. Siku moja, walipokuwa katika mbuga, walianza kugombana. Kwa vile hakukukuwa mutu yeyote wa kuwaamua, mumoja wao akamwua mwenzake. 7 Sasa wandugu zangu wote wamenigeuka mimi mujakazi wako. Wanataka nimutoe katika mikono yao yule mutoto aliyemwua mwenzake kusudi wamwue kwa kuyaangamiza maisha ya ndugu yake. Hivyo, watamwua huyu ambaye sasa ndiye murizi. Wakifanya hivyo, watazimisha kabisa tumaini langu lililobakia, na mume wangu hataachiwa jina wala muzao katika dunia.” 8 Mufalme akamwambia yule mwanamuke: “Rudi kwako nitaamuru jambo lako liangaliwe.” 9 Yule mwanamuke kutoka Tekoa akasema: “Bwana wangu mufalme, makosa yote yakuwe juu yangu na juu ya jamaa ya baba yangu. Hivyo, wewe na ufalme wako musikuwe na kosa.” 10 Mufalme akamwambia: “Mutu yeyote akikuchokoza umulete kwangu na hatakuja kukugusa tena.” 11 Yule mwanamuke akamwambia: “Tafazali, mufalme, uniombee kwa Yawe, Mungu wako, kusudi yule ndugu yangu ambaye angelipiza kisasi kutokana na mauaji ya mwana wangu hatafanya kosa lingine kubwa la kumwua yule mutoto wangu mwingine.” Mufalme Daudi akamwambia: “Kama vile Yawe anavyoishi, hakuna hata unywele mumoja wa mwana wako utakaoanguka chini.” 12 Yule mwanamuke akamwambia: “Ninakuomba, mimi mujakazi wako, uniruhusu niseme neno moja kwa ajili yako mufalme.” Mufalme akamwambia: “Sema”. 13 Yule mwanamuke akamwambia: “Kwa nini basi, umepanga kutenda uovu huu juu ya watu wa Mungu? Kulingana na uamuzi wako juu ya jambo hilo, wewe mwenyewe umejihukumu kuwa na kosa kwa sababu haumuruhusu mwana wako arudi kwa nyumba kutoka kule alikokimbilia. 14 Sisi wote tutakufa. Sisi ni kama maji yaliyomwangika chini ambayo hayawezi kuzoleka. Lakini Mungu hataki Abusaloma akufe sasa au aendelee kuishi mbali naye. 15 Mimi nimekuja kuzungumuza nawe, bwana wangu mufalme, maana wamenitisha. Basi, mimi mujakazi wako, niliwaza kwamba ni afazali nizungumuze na mufalme, labda atanitimizia mahitaji yangu mimi mujakazi wake. 16 Maana mufalme atanisikiliza na kuniokoa toka katika mikono ya mutu ambaye anataka kuniangamiza mimi pamoja na mwana wangu kutoka urizi wa Mungu. 17 Nami mujakazi wako nilifikiri hivi: ‘Neno la bwana wangu mufalme litanipa amani ndani ya moyo, maana wewe bwana wangu mufalme ni kama malaika wa Mungu katika kupambanua mazuri na mabaya.’ Yawe, Mungu wako, akuwe pamoja nawe.” 18 Halafu mufalme akamujibu yule mwanamuke: “Usinifiche jambo lolote nitakalokuuliza.” Yule mwanamuke akasema: “Sema bwana wangu mufalme.” 19 Mufalme akamwuliza: “Haukupatana na Yoabu katika jambo hili?” Yule mwanamuke akasema: “Kama vile unavyoishi mwenyewe bwana wangu mufalme, mutu hawezi kupita pembeni juu ya jambo ulilosema bwana wangu mufalme. Yoabu yule mutumishi wako ndiye aliyenituma. Ni yeye aliyeniambia maneno yote haya niliyokuambia mimi mujakazi wako. 20 Yoabu alifanya hivyo kwa kubadilisha mambo. Lakini, wewe bwana wangu, una hekima kama ya malaika wa Mungu hata unaweza kujua mambo yote yanayokuwa katika dunia.” 21 Kisha, mufalme akamwambia Yoabu: “Sasa sikiliza, ninakubali shauri lako. Kwenda umurudishe yule kijana Abusaloma.” 22 Yoabu alianguka uso mpaka chini, na kumutakia mufalme baraka, akasema: “Leo, mimi mutumishi wako, bwana wangu mufalme, ninajua kwamba nimepata kukubaliwa mbele yako, kwa kulikubali shauri langu.” 23 Kwa hiyo, Yoabu aliondoka, akaenda Gesuri kumuleta Abusaloma katika Yerusalema. 24 Lakini mufalme akasema: “Abusaloma aishi kwake. Asikuje hapa kuniona.” Kwa hiyo, Abusaloma akakuwa anaishi mbali, kwake na hakumwona mufalme Daudi. Abusaloma na mufalme Daudi wanapatana 25 Katika inchi yote ya Israeli, hakuna mutu yeyote aliyesifiwa kwa uzuri wa umbo kama Abusaloma. Tangia kwenye miguu mpaka kwenye kichwa, Abusaloma hakukuwa na kilema chochote. 26 Kila mara alipokata nywele zake, (na kila mwisho wa mwaka alikata nywele zake maana zilikuwa nzito), alipozipima, zilikuwa na uzito wa kilo mbili kulingana na vipimo vya kifalme. 27 Abusaloma alizaa watoto watatu wanaume pamoja na binti mumoja jina lake Tamari. Tamari alikuwa na sura nzuri. 28 Basi, Abusaloma aliishi Yerusalema kwa muda wa miaka miwili mizima bila kumwona mufalme Daudi. 29 Kisha, Abusaloma alimutumia Yoabu ujumbe, kusudi aende kwa mufalme kwa jina lake, lakini Yoabu akakataa. Abusaloma akatuma ujumbe mara ya pili lakini Yoabu akakataa. 30 Basi, Abusaloma akawaambia watumishi wake: “Muangalie, Yoabu ana shamba la shayiri karibu na langu. Muende mulichome kwa moto.” Kwa hiyo watumishi wa Abusaloma wakalichoma shamba la Yoabu kwa moto. 31 Yoabu akaenda kwa Abusaloma akamwuliza: “Kwa nini watumishi wako wamechoma shamba langu?” 32 Abusaloma akamujibu: “Nilikutumia ujumbe, ukuje huku kusudi nikutume kwa mufalme, umwulize: ‘Kwa nini niliondoka Gesuri? Ingekuwa bora kwangu kubaki kule.’ Sasa unisaidie nipate kumwona mufalme. Kama nina kosa basi, aniue!” 33 Kwa hiyo Yoabu akaenda na kumwelezea mufalme maneno hayo yote, naye akamwita Abusaloma. Abusaloma akaingia kwa mufalme, akaanguka uso mpaka chini mbele ya mufalme. Na mufalme akamubusu Abusaloma. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo