2 Mambo ya Siku 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ujenzi wa hekalu unaanza ( 1 Fal 6.1-38 ) 1 Kisha Solomono akaanza kujenga nyumba ya Yawe katika Yerusalema juu ya mulima Moria ambapo Yawe alimutokea Daudi baba yake, pahali ambapo Daudi alikuwa amepachagua, kwenye kiwanja cha kupepetea ngano cha Ornani Muyebusi. 2 Mufalme Solomono akaanza kujenga hekalu katika mwezi wa pili wa mwaka wa ine wa utawala wake. 3 Vipimo Solomono alivyotumia kwa kujenga nyumba ya Mungu, vilikuwa kama hivi: urefu metre makumi mbili na saba na upana metre kenda. 4 Chumba cha sehemu ya kuingilia kilikuwa na urefu wa metre kenda, sawa na upana wa nyumba hiyo, na urefu kwenda juu metre makumi tano na ine. Kuta zake zilifunikwa kwa zahabu safi upande wa ndani. 5 Baraza ilifunikwa kwa mbao za miberoshi. Kisha kwa zahabu safi na kuchorwa mifano ya miti ya ngazi na minyororo. 6 Mufalme Solomono aliipamba nyumba ya Yawe kwa mawe mazuri ya bei kali. Zahabu aliyotumia ilitoka katika inchi ya Parawaimu. 7 Alipakaa nyumba yote zahabu; nguzo zake, vizingiti vyake, kuta zake na milango yake. Vilevile wakachora kwenye kuta sanamu za makerubi. 8 Tena, alipatengeneza Pahali Patakatifu Sana. Urefu wake ulikuwa metre kenda, sawasawa na upana wake ambao vilevile ulikuwa metre tisa. Alitumia zaidi ya toni makumi mbili za zahabu kwa kupakaa ndani ya chumba kile. 9 Misumari aliyoitumia ilikuwa ya uzito wa grama mia tano na makumi saba za zahabu. Vilevile alipakaa vyumba vyote vya gorofi kwa zahabu. 10 Akatengeneza sanamu mbili za makerubi kwa mbao, akazipakaa kwa zahabu na kuziweka katika Pahali Patakatifu Sana. 11 Kila kerubi ilikuwa na mabawa mawili yenye urefu wa metre ine na nusu kwa jumla, metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano kila bawa. Bawa moja liligusa ukuta upande mumoja wa chumba na la pili liligusana na la kerubi wa pili. 12 Vilevile bawa moja la kerubi wa pili liligusa ukuta upande mwingine wa chumba na la pili likagusana na la kerubi wa kwanza katikati ya chumba. 13 Urefu wa mabawa mawili ya makerubi hawa ni metre ine na nusu. Yalisimama yakielekana, nyuso za makerubi zikielekea kwenye baraza. 14 Akatengeneza pazia kwa kitambaa cha kitani safi, cha rangi ya samawi, ya rangi nyekundu-nyeusi na nyekundu. Akalichora kwa michoro ya makerubi. Nguzo mbili za shaba ( 1 Fal 7.15-22 ) 15 Mufalme Solomono alitengeneza nguzo mbili za shaba, kila moja yenye urefu wa metre mia moja kumi na tano na nusu, akaziweka mbele ya nyumba. Kisha akatengeneza taji mbili, kila moja yenye urefu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili na tano, akaziweka juu ya nguzo zile. 16 Alitengeneza minyororo kwa mufano wa mikufu, akaiweka juu ya vichwa vya nguzo hizo, kisha akatengeneza mifano ya matunda aina ya makomamanga mia moja, akayaweka juu ya minyororo hiyo. 17 Akazisimamisha nguzo zile kwenye baraza ya hekalu, moja upande wa kusini, na ingine upande wa kaskazini; ile ya upande wa kusini akaiita Yakini, na ya upande wa kaskazini akaiita Boazi. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo