2 Mambo ya Siku 17 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yosafati anawekwa kuwa mufalme 1 Naye Yosafati mwana wake akatawala pahali pa baba yake Asa, akajiimarisha juu ya inchi ya Israeli. 2 Aliweka majeshi katika miji yote ya inchi ya Yuda yenye kuta, na katika maeneo mengine ya Yuda akaweka waaskari walinzi, na katika miji ya Efuraimu ambayo baba yake Asa aliiteka. 3 Yawe alikuwa pamoja na Yosafati kwa sababu alifuata njia za kwanza za babu yake Daudi, wala hakumwabudu mungu Bali. 4 Yeye alimutafuta Mungu wa babu yake na kutii amri zake, wala hakufuata matendo ya Israeli. 5 Yawe, akauimarisha ufalme wa Yuda katika mikono ya Yosafati, nao watu wote wakamuletea zawadi, akatajirika sana na kuheshimika. 6 Alipenda sana ndani ya moyo kumutumikia Yawe, na zaidi ya hayo, alipaharibu pahali pote pa kuabudia miungu mingine na sanamu za Ashera, mungu wa kike, katika inchi ya Yuda. 7 Katika mwaka wa tatu wa utawala wake, Yosafati akawatuma wakubwa hawa wafundishe katika miji ya Yuda: Ben-Haili, Obadia, Zakaria, Netaneli na Mikaya. 8 Walawi kenda na Makuhani wawili wakaandamana nao. Walawi hao walikuwa Semaya, Netania, Zebadia, Asaeli, Semiramoti, Yonatani, Adonia, Tobia na Tobu-Adonia; nao makuhani walikuwa Elisama na Yoramu. 9 Walitwaa kitabu cha Sheria ya Yawe, wakazunguka nacho katika miji yote ya Yuda wakifundisha watu. Ukubwa wa Yosafati 10 Yawe akaogopesha falme zote jirani za inchi ya Yuda, zikaogopa kupigana vita na Yosafati. 11 Vilevile Wafilistini wamoja wakamuletea Yosafati zawadi pamoja na feza nyingi na Waarabu wengine nao wakamuletea kondoo dume elfu saba na mia saba, na mbuzi dume elfu saba na mia saba. 12 Kwa hiyo Yosafati akaendelea kuwa mukubwa zaidi. Akajenga makimbilio na miji ya hazina. 13 Naye alikuwa na hazina kubwa katika miji ya Yuda. Kule Yerusalema, aliweka waaskari wa jeshi mashujaa. 14 Hii ndiyo hesabu yao kulingana na ukoo za babu zao: Adina alikuwa jemadari wa vikundi vya waaskari elfu wa kabila la Yuda. Chini yake, kulikuwa waaskari elfu mia tatu. 15 Wa pili nyuma yake katika cheo alikuwa jemadari Yohanani, akiwa na waaskari elfu mia mbili na makumi nane, 16 na wa tatu alikuwa Amasia mwana wa Sikiri, akiwa na waaskari mashujaa elfu mia mbili. Amasia alijitolea kwa mapenzi yake kumutumikia Yawe. 17 Jemadari wa vikundi vya waaskari waliotoka katika kabila la Benjamina alikuwa Eliada, mutu hodari, naye alikuwa na waaskari elfu mia mbili, wenye pinde na ngao. 18 Wa pili nyuma yake alikuwa Yozabadi, aliyekuwa na waaskari elfu mia moja makumi nane waliojitayarisha kwa vita. 19 Watu wote hao walimutumikia mufalme kule Yerusalema, na zaidi ya hayo, aliweka waaskari wengine katika miji ile mingine yenye makimbilio kote katika inchi ya Yuda. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo