2 Mambo ya Siku 14 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mufalme Asa anawashinda Waetiopia 1 Asa akatenda mambo yanayokuwa mazuri na sawa mbele ya Yawe, Mungu wake. 2 Aliondoa katika inchi mazabahu za kigeni na pahali pa kuabudia miungu mingine, akabomoa minara na kukatakata sanamu za Ashera. 3 Aliwaamuru watu wa Yuda wamutafute Yawe, Mungu wa babu zao, na kutii Sheria na amri. 4 Vilevile aliondoa pahali pote pa kuabudia miungu mingine na meza za kufukizia ubani kutoka katika miji yote ya Yuda; halafu ufalme wake ulikuwa na amani chini ya utawala wake. 5 Alijenga miji yenye kuta za kuiimarisha inchi ya Yuda wakati ule wa amani, na kwa muda wa miaka ile, hapakutokea vita kwa maana Yawe alimupa amani. 6 Naye Asa akawaambia watu wa Yuda: “Tujenge miji hii na kuizungushia kuta na minara, milango yenye vifungio vya vyuma. Inchi ingali katika mikono yetu kwa maana tumetenda mapenzi ya Yawe, Mungu wetu, naye ametupatia amani pande zote.” Basi wakajenga na kufanikiwa. 7 Mufalme Asa alikuwa na jeshi la waaskari elfu mia tatu kutoka Yuda, wenye ngao na mikuki, na wengine elfu mia mbili na makumi nane kutoka katika kabila la Benjamina, wenye ngao na pinde. Wote walikuwa watu mashujaa sana. 8 Zera, Mwetiopia alishambulia inchi ya Yuda akiwa na jeshi la waaskari milioni moja na magari mia tatu, akasonga mbele mpaka Maresa. 9 Asa alitoka akaenda kupigana naye. Pande zote mbili zilijipanga katika Bonde la Sefata karibu na Maresa. 10 Hapo Asa akamulilia Yawe, Mungu wake, akisema: “Ee Yawe, hakuna mwingine kama wewe, mwenye uwezo wa kusaidia jeshi likuwe zaifu au lenye nguvu. Utusaidie, ee Yawe, Mungu wetu, kwa sababu sisi tunakutegemea wewe, na kwa jina lako tumekuja kupigana vita na jeshi hili kubwa ajabu. Ee Yawe, wewe ndiwe Mungu wetu; usimuruhusu mwanadamu yeyote ashindane nawe.” 11 Yawe akawashinda Waetiopia mbele ya Asa na jeshi lake la watu wa Yuda. Waetiopia wakakimbia. 12 Asa pamoja na waaskari wake wakawafuatilia mpaka Gerari, wakawaua Waetiopia wengi sana, hapakubaki hata mumoja, maana walikuwa wamekwisha kushindwa na Yawe pamoja na jeshi lake. Jeshi la Yuda likateka vitu vingi sana. 13 Likaharibu miji yote iliyokuwa kandokando ya Gerari, kwa kuwa watu waliokuwa katika miji ile, walipatwa na hofu ya Yawe. Likabeba mali nyingi kutoka katika miji ile, kwa sababu kulikuwa mali mengi sana. 14 Likashambulia vilevile wachungaji, likachukua kondoo wengi na ngamia. Kisha likarudia Yerusalema. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo