1 Wafalme 22 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Nabii Mikaya anamwonya Ahabu ( 2 Sik 18.2-27 ) 1 Kwa muda wa miaka mitatu hivi, kulikuwa amani kati ya Israeli na Aramu. 2 Lakini katika mwaka wa tatu, Yosafati mufalme wa Yuda alifika kumutembelea Ahabu mufalme wa Israeli. 3 Ahabu akawaambia watumishi wake: “Hamujui kwamba muji wa Ramoti-Gileadi ni mali yetu? Mbona basi tunajiikalia tu bila kuunyanganya kutoka kwa mufalme wa Aramu?” 4 Kisha akamwuliza Yosafati: “Utaandamana nami kwa kupigana kule Ramoti-Gileadi?” Naye Yosafati akamujibu mufalme wa Israeli: “Ndiyo, mimi na wewe ni mutu mumoja, watu wangu ni watu wako, farasi wangu ni farasi wako.” 5 Kisha Yosafati aliendelea kumwambia mufalme wa Israeli: “Lakini, kwanza umwulize Yawe shauri.” 6 Basi, Ahabu akakusanya manabii yapata mia ine, akawauliza: “Niende au nisiende kushambulia Ramoti-Gileadi?” Nao wakamujibu: “Kwenda! Yawe atakupatia ushindi.” 7 Lakini, Yosafati akasema: “Hapa hakuna nabii mwingine wa Yawe ambaye tunaweza kumwomba shauri?” 8 Naye mufalme wa Israeli akamujibu Yosafati: “Kungali mumoja, Mikaya mwana wa Imula. Yeye tunaweza kumwomba shauri la Yawe. Lakini ninamuchukia sana kwa sababu yeye, hatabiri jambo zuri juu yangu hata kidogo, lakini baya tu.” Yosafati akamwambia: “Si vizuri kwa mufalme kusema hivyo.” 9 Basi, Ahabu mufalme wa Israeli akamwita mutumishi mumoja, akamwamuru: “Haraka! Kwenda umulete Mikaya mwana wa Imula.” 10 Wakati ule, mufalme wa Israeli pamoja na Yosafati mufalme wa Yuda walikuwa wakiikaa katika viti vyao vya kifalme, wakiikaa kwenye kiwanja cha kupepetea ngano kwenye mulango wa kuingilia katika muji wa Samaria, nao walikuwa wakivaa nguo zao za kifalme. Wakati ule manabii wote wakakuwa wanatabiri mbele yao. 11 Kisha mumoja wa manabii hao, Zedekia mwana wa Kenana, akajitengenezea pembe za chuma akasema: “Yawe anasema hivi: ‘Kwa pembe hizi, utawarudisha nyuma Waaramu na kuwaangamiza.’ ” 12 Hata wale manabii wengine wote wakatabiri vile vile, wakasema: “Kwenda uushambulie muji wa Ramoti-Gileadi, utashinda! Yawe atautia katika mikono yako.” 13 Wakati ule, yule mutumishi aliyetumwa kwenda kwa Mikaya, akamwambia: “Manabii wengine wote kwa pamoja, wamemutabiria mufalme ushindi. Tafazali, nawe vilevile ufanye kama wao, umutabirie mazuri.” 14 Lakini Mikaya akamujibu: “Kama vile Yawe anavyoishi, mimi nitasema tu yale Yawe atakayoniambia.” 15 Basi, Mikaya alipofika mbele ya mufalme, mufalme akamwuliza: “Twende kupigana vita kule Ramoti-Gileadi au tusiende?” Naye alimujibu: “Kwenda na ufanikiwe, naye Yawe atautia katika mikono yako.” 16 Lakini mufalme akamwambia: “Nitakuapisha mara ngapi kwamba unaposema nami kwa jina la Yawe, unapaswa kuniambia ukweli mutupu?” 17 Halafu, Mikaya akasema: “Niliona watu wote wa Israeli wametawanyika juu ya milima kama kondoo wasiokuwa na muchungaji. Naye Yawe akasema: ‘Watu hawa hawana kiongozi. Basi warudi kila mutu kwake kwa amani.’ ” 18 Hapo, mufalme wa Israeli akamwuliza Yosafati: “Sikukuambia hatatabiri mazuri hata kidogo juu yangu lakini mabaya tu?” 19 Kisha Mikaya akasema: “Sasa sikia neno la Yawe: Nilimwona Yawe akiikaa katika kiti chake cha kifalme, na jeshi lote la mbinguni likisimama pembeni yake, upande wake wa kuume na wa kushoto. 20 Halafu Yawe akauliza: ‘Ni nani atakayemushawishi Ahabu aende aangamie kule Ramoti-Gileadi?’ Kila mumoja akajibu namna alivyofikiri. 21 Kisha pepo mumoja akajitokeza mbele ya Yawe, akasema: ‘Mimi nitamushawishi.’ 22 Yawe akamwuliza: ‘Kwa namna gani?’ Naye akajibu: ‘Nitakwenda na kuwasukuma manabii wake wote waseme uongo.’ Yawe akamwambia: ‘Wewe utamushawishi na utashinda; basi, kwenda ufanye hivyo.’ 23 Basi, ndivyo inavyokuwa: Yawe amewasukuma hawa manabii wako wote waseme uongo. Yawe amesema mabaya juu yako!” 24 Zedekia mwana wa Kenana akamukaribia Mikaya, akamupiga kofi kwenye shavu na kumwuliza: “Tangu wakati gani Roho wa Yawe ameniacha mimi, na kuanza kusema nawe?” 25 Mikaya akamujibu: “Siku utakapoingia katika chumba cha ndani kwa kujificha, ndipo utakapojua.” 26 Naye mufalme wa Israeli akatoa amri: “Mumukamate Mikaya. Mumupeleke kwa Amoni mukubwa wa muji na kwa Yoasi mwana wa mufalme. 27 Uwaambie wamutie katika gereza na kumukulisha mukate kidogo na maji, mpaka nitakaporudi salama.” 28 Halafu Mikaya alisema: “Ukirudi salama basi, utajua kwamba Yawe hakusema nami.” Kisha akaendelea kusema: “Musikilize enyi watu wote!” Kifo cha Ahabu ( 2 Sik 18.28-34 ) 29 Basi, mufalme wa Israeli akaenda pamoja na mufalme Yosafati wa Yuda kuushambulia muji wa Ramoti-Gileadi. 30 Mufalme wa Israeli akamwambia Yosafati: “Mimi nitavaa nguo zisizokuwa za kifalme na kuingia katika vita lakini wewe utavaa nguo zako za kifalme.” Hivyo mufalme wa Israeli akaenda kwenye vita bila kuvaa nguo za kifalme. 31 Mufalme wa Aramu alikuwa amewaamuru viongozi wake makumi tatu na wawili waliosimamia magari yake ya vita, akisema: “Musishambulie mutu yeyote, mukubwa au mudogo, lakini tu mufalme wa Israeli.” 32 Nyuma, viongozi hao walipomwona Yosafati, walisema: “Kweli, huyu ndiye mufalme wa Israeli.” Kwa hiyo, walimwelekea, wakamushambulia, lakini Yosafati akapiga kelele. 33 Viongozi walipotambua kwamba hakukuwa mufalme wa Israeli waliacha kumushambulia, wakarudia. 34 Lakini, askari mumoja wa Aramu akauvuta upinde wake kwa kubahatisha, akamupiga mushale mufalme wa Israeli katika maunganio ya nguo zake za chuma za kukinga kifua. Hapo Ahabu akamwambia kiongozi wa gari lake la vita: “Geuza gari uniondoe katika vita. Nimeumizwa!” 35 Na mapigano siku hiyo yakazidi kuwa makali, naye mufalme akiegemeshwa ndani ya gari, akiwaelekea Waaramu. Ilipofika magaribi, akakufa. Damu ikakuwa inamutoka kwenye kidonda chake na kutiririka mpaka chini ya gari. 36 Jua liliposhuka, amri ikatolewa: “Kila mutu arudie kwake! Kila mutu arudie kwake!” 37 Mufalme Ahabu alikufa na maiti yake ilipelekwa Samaria, ikazikwa kule. 38 Gari lake la vita walilisafisha katika kisima cha Samaria, imbwa wakailamba damu yake, nao makahaba wakaoga mule, sawa kabisa na neno Yawe alilosema. 39 Mambo mengine ya Ahabu, yote aliyofanya, na jinsi alivyojenga na kupamba nyumba yake kwa pembe, na miji yote aliyojenga, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Israeli. 40 Ahabu alipokufa, mwana wake Ahazia alitawala kwa pahali pake. Yosafati, mufalme wa Yuda ( 2 Sik 20.31–21.1 ) 41 Katika mwaka wa ine wa utawala wa mufalme Ahabu wa Israeli, Yosafati mwana wa Asa alianza kutawala Yuda. 42 Yosafati alikuwa na umri wa miaka makumi tatu na mitano alipoanza kutawala. Alitawala akiwa Yerusalema kwa muda wa miaka makumi mbili na mitano. Mama yake aliitwa Azuba binti ya Silihi. 43 Alitenda mema mbele ya Yawe kama vile baba yake Asa alivyofanya. 44 Lakini hakuharibu nafasi ya kutambikia juu ya vilima. Watu waliendelea kutambikia na kufukiza ubani kwa nafasi ile. 45 Yosafati vilevile, alifanya mapatano ya amani na mufalme wa Israeli. 46 Matendo mengine ya Yosafati, ushujaa wake na vita alivyopigana, yote yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Siku za Wafalme wa Yuda. 47 Waasherati wote wa kidini waliobaki tangu nyakati za baba yake Asa, Yosafati aliwaondoa katika inchi. 48 Katika inchi ya Edomu, hakukuwa mufalme. Inchi hiyo ilitawaliwa na musimamizi. 49 Mufalme Yosafati alitengeneza mashua za kwenda Ofiri kuleta zahabu, lakini hazikufika kwa sababu zilivunjikavunjika kule Esioni-Geberi. 50 Basi, Ahazia mwana wa Ahabu akamwambia Yosafati: “Uwaache watumishi wangu wasafiri pamoja na watumishi wako katika mashua.” Lakini Yosafati hakukubali jambo hilo. 51 Kwa mwisho, Yosafati akakufa, akazikwa pamoja na babu zake katika makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi babu yake. Naye Yoramu mwana wake akatawala kwa pahali pake. Ahazia, mufalme wa Israeli 52 Katika mwaka wa kumi na saba wa utawala wa Yosafati mufalme wa Yuda, Ahazia mwana wa Ahabu alianza kutawala Israeli. Alitawala kwa muda wa miaka miwili, akiwa Samaria. 53 Ahazia alitenda maovu mbele ya Yawe; alifuata mwenendo wa baba yake na mwenendo wa mama yake Yezebeli, na wa Yeroboamu mwana wa Nebati ambaye aliwasukuma watu wa Israeli watende zambi. 54 Alimutumikia na kumwabudu Bali, akamukasirikisha Yawe, Mungu wa Israeli, kwa kila jambo kama vile baba yake alivyofanya. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo