1 Wafalme 21 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maneno ya shamba la Naboti 1 Nyuma ya mambo hayo, Naboti wa muji wa Yezereheli alikuwa na shamba lake la mizabibu kule Yezereheli, karibu na nyumba ya Ahabu, mufalme wa Samaria. 2 Basi, siku moja, Ahabu akamwambia Naboti: “Unipe shamba lako la mizabibu nilifanye shamba la mboga, kwa sababu liko karibu na nyumba yangu. Nitakupa shamba lingine zuri zaidi, au ukitaka nitakulipa feza sawasawa na bei yake.” 3 Lakini, Naboti akamujibu: “Jambo la kukupa wewe urizi nilioupata kwa wazee wangu, Yawe alipitishe mbali.” 4 Hapo, Ahabu akarudi kwake akijaa chuki na huzuni nyingi, kwa sababu Naboti wa Yezereheli alimwambia kwamba hatamupa kile alichorizi kutoka kwa wazee wake. Basi, akalala kwenye kitanda, akaficha uso wake na kukataa chakula. 5 Yezebeli, muke wake, akamwendea na kumwuliza: “Mbona umejaa huzuni ndani ya moyo hata kula haukuli?” 6 Naye akamwambia: “Kwa sababu nilizungumuza na Naboti wa Yezereheli, nikataka aniuzishie shamba lake la mizabibu, au kama akipenda nimupe shamba lingine pahali pa lile. Lakini yeye akaniambia: ‘Sitakupa shamba langu la mizabibu.’ ” 7 Hapo, Yezebeli, muke wake, akamwambia: “Anayetawala Israeli ni nani? Si ni wewe? Amuka, ukule na uchangamuke. Mimi peke yangu nitakupa shamba la mizabibu la Naboti wa Yezereheli.” 8 Basi, Yezebeli akaandika barua kwa jina la Ahabu na kuzipiga muhuri wa mufalme. Kisha akapeleka barua hizo kwa wazee na watu wenye heshima walioishi na Naboti kule katika muji. 9 Barua zenyewe ziliandikwa hivi: “Mutangaze kwa watu kwa kufanya sikukuu ya kufunga kula, mukutane na kumupa Naboti nafasi ya heshima kati ya watu. 10 Kisha, mutafute watenda maovu wawili wapate kumushuhudia na kumushitaki wakisema: ‘Wewe umemutukana Mungu na mufalme.’ Kisha mumupeleke inje, mumwue kwa kumutupia mawe!” 11 Basi, wakaaji wenzake na Naboti, wazee na watu wenye heshima wa muji wa Yezereheli wakafanya kama vile Yezebeli alivyowaagiza. Kwa kufuatana na barua alizowatumia, 12 wakatangaza sikukuu ya kufunga kula, wakakutana na kumuweka Naboti kwenye nafasi ya heshima kati ya watu. 13 Wale watenda maovu wawili wakaikaa kwa kumushuhudia Naboti, kisha wakamushitaki mbele ya watu wote wakisema: “Naboti amemutukana Mungu na mufalme.” Basi, Naboti akapelekwa inje ya muji, akauawa kwa kutupiwa mawe. 14 Kisha, Yezebeli akapelekewa habari kwamba Naboti amekwisha uawa kwa kutupiwa mawe. 15 Mara tu Yezebeli alipopata habari kwamba Naboti amekwisha kufa kwa kutupiwa mawe, akamwambia Ahabu: “Simama! Kwenda utwae lile shamba la mizabibu la Naboti wa Yezereheli ambalo alikataa kukuuzishia. Naboti hayuko muzima tena; amekwisha kufa.” 16 Mara tu Ahabu aliposikia kwamba Naboti amekwisha kufa, akasimama na kwenda kulitwaa shamba la mizabibu la Naboti. Nabii Elia anamukaripia Ahabu 17 Basi, neno la Yawe lilimufikia Elia wa Tisibe kusema hivi: 18 “Simama uende kukutana na Ahabu mufalme wa Israeli, ambaye yuko Samaria. Utamukuta katika shamba la mizabibu la Naboti kwa kulitwaa. 19 Umwambie, Yawe anasema hivi: ‘Umeua na kutwaa mali yake vilevile?’ Umwambie Yawe anasema hivi: ‘Pahali pale imbwa walipoilambulia damu ya Naboti, ndipo watakapoilambulia damu yako.’ ” 20 Basi, Ahabu alipomwona Elia, akasema: “Ewe adui yangu, umeninasa tena?” Elia akamujibu: “Ndiyo! Nimekunasa, kwa sababu wewe umekusudia kabisa kutenda maovu mbele ya Yawe. 21 Basi! Yawe anasema hivi: ‘Hakika, nitakuletea maangamizi. Nitakuletea hasa wewe na kuangamiza kila mwanaume wa ukoo wako katika Israeli, akuwe mutumwa au huru. 22 Jamaa yako nitaifanya kama jamaa ya Yeroboamu mwana wa Nebati, na kama jamaa ya Basha mwana wa Ahiya, kwa sababu umeiwasha hasira yangu na kuwasukuma watu wa Israeli watende zambi.’ 23 Tena, Yawe anasema hivi juu ya Yezebeli: ‘Imbwa wataukula mwili wa Yezebeli humuhumu katika muji wa Yezereheli. 24 Hakika, mutu yeyote wa jamaa yake atakayekufia ndani ya muji, imbwa watamukula; na mutu yeyote atakayekufia katika shamba, ndege watamukula.’ ” 25 Hakuna mutu aliyekusudia kutenda maovu mbele ya Yawe kama Ahabu, ambaye alishawishiwa na Yezebeli, muke wake. 26 Alitenda machukizo kwa kuabudu sanamu za miungu kama vile Waamori walivyofanya ambao zamani Yawe aliwafukuza mbele ya watu wa Israeli. 27 Lakini, Ahabu aliposikia maneno hayo, akapasua nguo zake, akavaa gunia peke yake, akafunga, akakuwa analala na gunia, na kwenda huko na huko kwa huzuni. 28 Basi, neno la Yawe lilimufikia Elia wa Tisibe kusema hivi: 29 “Umeona jinsi Ahabu alivyojinyenyekeza mbele yangu? Basi, kwa sababu amejinyenyekeza, sitaleta yale maangamizi atakapokuwa angali anaishi, lakini nyakati za utawala wa mwana wake nitaiangamiza jamaa ya Ahabu.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo