1 Timoteo 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maagizo juu ya maombi 1 Mbele ya yote, ninawaonya ninyi kuwaombea watu wote. Muombe Mungu awasaidie na kuwabariki, na mumushukuru kwa ajili yao. 2 Inafaa kuombea wafalme na watu wenye mamlaka kusudi tupate kuishi katika ukimya na amani katika kushikamana na ibada na katika mwenendo safi. 3 Nalo jambo hilo ni zuri na lenye kupendeza Mungu Mwokozi wetu, 4 anayetaka watu wote waokolewe na kuweza kutambua ukweli. 5 Kwa maana kuna Mungu mumoja tu, na kuna mupatanishi mumoja tu kati ya Mungu na watu, ni yule mutu, Kristo Yesu, 6 aliyejitoa mwenyewe kusudi awakomboe watu wote. Na huo ni ushuhuda kwa wakati uliopangwa, kwamba Mungu anataka kuwaokoa watu wake. 7 Ni kwa hiyo nimewekwa kuwa mujumbe na mutume kwa kuwafundisha watu wa mataifa mengine kusudi wapate kumwamini Mungu na kutambua ukweli. Mimi ninasema ukweli wala si uongo. 8 Basi, ninataka watu waombe Mungu wakiinua mikono juu, ikiwa imetakaswa, nao wafanye vile bila kasirani wala ubishi. 9 Ninataka vilevile wanawake wavae kwa namna inayostahili. Inafaa wajipambe kwa adabu na kwa ukadirifu, si kwa namna mbalimbali za urembo za kusuka nywele, wala kwa zahabu, wala kwa ushanga au nguo za bei kali. 10 Lakini kujipamba kwao kuwe matendo mema yanayostahili kutendwa na wanawake wanaojidai kwamba wanajitoa kwa kumwabudu Mungu. 11 Wanawake wanapaswa kusikiliza mafundisho katika ukimya na utii kabisa. 12 Lakini simupatii mwanamuke ruhusa ya kufundisha, wala ya kumutawala mwanaume, lakini akae katika ukimya. 13 Kwa maana, Adamu ndiye aliyeumbwa wa kwanza, na kisha Eva. 14 Na si Adamu aliyedanganywa, lakini ni mwanamuke ndiye aliyedanganywa na kuasi agizo la Mungu. 15 Ingawa hivi mwanamuke ataokolewa kwa kuzaa watoto, kama akidumu katika imani, upendo na utakatifu na kuwa mukadirifu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo