1 Samweli 25 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Samweli anakufa 1 Sasa, Samweli akakufa. Nao Waisraeli wote wakakusanyika kwa kumwomboleza. Wakamuzika kwenye nyumba yake kule Rama. Kisha Daudi akaenda zake kwenye jangwa za Parani. Daudi na Abigaili 2 Kulikuwa mutu mumoja kule katika muji wa Maoni ambaye alikuwa na biashara ya kondoo katika muji wa Karmeli. Kule Karmeli alifuga kondoo wake na kuwakata manyoya. Alikuwa tajiri sana. Alikuwa na kondoo elfu tatu na mbuzi elfu moja. 3 Mutu yule aliitwa Nabali na muke wake aliitwa Abigaili. Abigaili alikuwa mwanamuke mwenye akili na sura nzuri. Lakini Nabali alikuwa mutu wa chuki na mutenda maovu; tena alikuwa wa ukoo wa Kalebu. 4 Basi, Daudi akiwa kule katika jangwa alisikia kwamba Nabali alikuwa anawakata kondoo wake manyoya kule Karmeli. 5 Kwa hiyo, akawatuma vijana kumi, akawaambia: “Mwende kwa Nabali kule Karmeli mumupelekee salamu zangu. 6 Mutamwambia kwamba Daudi anakusalimia hivi: ‘Amani ikuwe kwako, kwa jamaa yako na yote unayokuwa nayo. 7 Nimesikia kwamba unawakata kondoo wako manyoya. Ninataka ujue kwamba wachungaji wako walikuwa pamoja nasi, nasi hatukuwazuru. Tena muda wote walipokuwa pamoja nasi katika muji wa Karmeli, hawakukosa kitu chochote. 8 Ukiwauliza, watakuambia. Sasa ninakuomba vijana wangu hawa wapate kukubaliwa mbele yako, maana tumefika wakati wa sikukuu. Tafazali uwapatie kitu chochote unachokuwa nacho watumishi wako hawa nami mwana wako Daudi.’ ” 9 Wale vijana wa Daudi walikwenda na kumwambia Nabali kama walivyoagizwa na Daudi. Halafu wakangojea kidogo. 10 Kisha Nabali akawajibu watumishi wa Daudi: “Daudi ni nani? Mwana wa Yese ni nani? Siku hizi kuna watumishi wengi wanaowakimbia wabwana zao. 11 Nikamate mikate yangu, maji yangu na nyama niliyowachinjia wakata manyoya ya kondoo wangu na kuwapa watu ambao sijui hata wanatoka wapi?” 12 Basi, wale vijana wa Daudi walirudi na kumwambia Daudi namna walivyojibiwa. 13 Kwa hiyo Daudi akawaambia watu wake: “Kila mutu apakatie upanga wake kwenye kiuno.” Kila mutu akapakatia upanga wake, na Daudi vilevile akapakatia upanga wake. Watu yapata mia ine wakamufuata Daudi na watu mia mbili wakabaki na mizigo. 14 Kijana mumoja wa Nabali, akamwambia Abigaili, muke wa Nabali: “Daudi alituma wajumbe toka katika jangwa kuja kumusalimia bwana wetu. Lakini yeye aliwatukana. 15 Lakini watu hao walikuwa wema sana kwetu, hawakutuzuru; na wakati wote tulipokuwa nao kule katika jangwa hatukukosa kitu chochote. 16 Kwetu, walikuwa kama ukuta wa ulinzi usiku na muchana muda wote tulipokuwa tunawachunga kondoo. 17 Sasa ufikiri juu ya jambo hili na uamue la kufanya. Jambo hili linaweza kuleta hasara kwa bwana wetu na jamaa yake yote. Yeye ni mutu mubaya na hakuna anayeweza kusema naye.” 18 Abigaili akafanya haraka, akatwaa mikate mia mbili, mifuko miwili ya ngozi ya mbuzi yenye kujaa divai, kondoo watano waliotayarishwa vizuri, kilo kumi na saba za ngano zenye kukaangwa, vishada mia moja vya zabibu zenye kukauka, mikate ya tini mia mbili, na vitu hivi vyote akavipakia juu ya punda. 19 Akamwambia yule kijana wake: “Utangulie! Mimi nitakufuata.” Lakini hakumwambia mume wake neno lolote. 20 Alipokuwa anateremuka, akipanda juu ya punda wake, na kukingwa na mulima upande mumoja, akakutana kwa rafla na Daudi na watu wake wakiwa wanaelekea upande anakotoka. 21 Daudi alikuwa akifikiri: “Mimi nimekuwa nikilinda mali yote ya Nabali katika jangwa bila faida yoyote na hakuna kitu chake chochote kilichopotea, naye amenilipa mabaya kwa mazuri niliyomutendea. 22 Mungu aniue mimi ikiwa kesho asubui nitakuwa sijawaua wanaume wake wote.” 23 Abigaili alipomwona tu Daudi, akashuka mara moja kutoka juu ya punda wake, na kuinama mbele ya Daudi mpaka uso wake ukagusa chini. 24 Alijitupa kwenye miguu ya Daudi na kumwambia: “Bwana wangu, kosa lote likuwe juu yangu tu. Ninakuomba niongee nawe mimi mujakazi wako. Ninakuomba usikilize maneno ya mujakazi wako. 25 Usimwangalie Nabali ambaye ni mutu mubaya. Maana jina lake la Nabali linamustahili. Yeye anaitwa Nabali; na kweli yeye ni mutu mupumbafu. Bwana wangu, wale vijana wako ulipowatuma, mimi mujakazi wako sikuwaona. 26 Sasa bwana wangu, kama vile Yawe anavyoishi na kama vile unavyoishi, unaona kwamba Yawe amekuzuia kulipiza kisasi kwa kumwanga damu na hivyo upate kuwa na kosa. Uwaache waadui zako na wale wote wanaokutakia mabaya wakuwe wapumbafu kama Nabali. 27 Bwana wangu, ninakuomba upokee zawadi hii niliyokuletea, na uwape vijana wanaokufuata. 28 Ninakuomba unisamehe mimi mujakazi wako. Yawe atakupa jamaa imara kwa sababu, wewe bwana wangu, unapigana vita ya Yawe. Wakati wote wa maisha yako usipatikane na ubaya wowote. 29 Kukitokea watu wanaokufuatilia na kutaka kuyaangamiza maisha yako, Yawe, Mungu wako, atayalinda maisha yako pamoja na watu wanaokuwa wazima. Lakini atayatupilia mbali maisha ya waadui zako, kama vile mutu anavyotupa jiwe kwa mujeledi. 30 Nyuma ya Yawe kukutendea mazuri yote aliyokuahidi, na kukuchagua kuwa mutawala wa Israeli, 31 wewe bwana wangu, hautakuwa na sababu ya kujuta wala kuhukumiwa na zamiri kutokana na kumwanga damu bila sababu kwa kujilipiza kisasi. Lakini, Yawe atakapokuwa amekutendea vizuri, ninakuomba, bwana wangu, unikumbuke mimi mujakazi wako.” 32 Daudi akamwambia Abigaili: “Atukuzwe Yawe, Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo kukutana nami. 33 Umutukuze Yawe aliyekupa hekima kwa kunizuia kuwa na kosa la umwangaji wa damu na kujilipiza kisasi mimi mwenyewe. 34 Kwa hakika, kama Yawe, Mungu wa Israeli, anavyoishi, amenizuia kukuzuru. Usingefanya haraka kuja kukutana nami, kwa hakika, kesho asubui hakuna mwanaume yeyote wa Nabali ambaye angebaki.” 35 Kisha, Daudi akapokea vitu vyote ambavyo Abigaili alikuwa amemuletea, akamwambia Abigaili: “Rudi kwako na amani. Mimi nimeyasikia uliyosema, na ombi lako nimelipokea.” 36 Abigaili aliporudi kwake, alimukuta Nabali akifanya karamu kubwa katika nyumba yake kama ya kifalme. Nabali alikuwa akifurahi sana ndani ya moyo maana alikuwa amelewa sana. Kwa hiyo hakumwambia neno lolote mpaka asubui. 37 Asubui, Abigaili alipoona kwamba divai imemutoka mume wake, alimwelezea mambo yote, na palepale Nabali akapooza, akakuwa kama jiwe. 38 Kisha siku kumi, Yawe alimupiga Nabali akakufa. 39 Daudi aliposikia kwamba Nabali amekufa, alisema: “Atukuzwe Yawe ambaye amemulipiza kisasi Nabali kwa kunitukana, naye Yawe ameniepusha mimi mutumishi wake kutenda maovu. Yawe amemwazibu Nabali kwa uovu wake.” Kisha Daudi alituma watu kwa kumuchumbilia Abigaili akuwe muke wake. 40 Watumishi wa Daudi walipofika kwa Abigaili kule Karmeli, wakamwambia: “Daudi ametutuma kukutwaa kusudi ukuwe muke wake.” 41 Abigaili alisimama, na kuinama mbele yao uso mpaka chini, akasema: “Mimi ni mujakazi tu. Niko tayari kunawisha miguu ya watumishi wa bwana wangu.” 42 Abigaili alifanya haraka, akasimama na kupanda juu ya punda wake, akifuatana na wajakazi wake watano, akaenda na watumishi wa Daudi. Akakuwa muke wake. 43 Tena Daudi alimwoa Ahinoamu wa Yezereheli. Hivyo hao wawili wakakuwa wake zake. 44 Wakati huo, Saulo alikuwa amemwoesha binti yake Mikali, ambaye alikuwa muke wa Daudi, kwa Palti mwana wa Laisi, wa muji wa Galimu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo