1 Samweli 23 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Daudi anauokoa muji wa Keila 1 Kisha Daudi aliambiwa: “Sikiliza, Wafilistini wanaushambulia muji wa Keila na kunyanganya ngano kwenye viwanja vya kupepetea.” 2 Basi, Daudi akamwomba Yawe shauri: “Niende kuwashambulia Wafilistini hawa?” Yawe akamujibu: “Ndiyo, kwenda kuwashambulia Wafilistini na kuuokoa muji wa Keila.” 3 Lakini watu wa Daudi wakamwambia: “Kama tukiwa hapahapa katikati ya inchi ya Yuda tunaogopa, itakuwa namna gani basi tukienda Keila na kushambulia waaskari wa Wafilistini?” 4 Daudi akamwomba tena Yawe shauri, naye Yawe akamwambia: “Simama uende Keila maana nitawatia Wafilistini katika mikono yako.” 5 Basi, Daudi akaenda Keila pamoja na watu wake, na kule akapigana na Wafilistini, akawaua Wafilistini wengi na kunyanganya ngombe wengi. Kwa hiyo Daudi aliwaokoa wakaaji wa Keila. 6 Abiatari mwana wa Ahimeleki, alipokimbilia kwa Daudi kule Keila, alikwenda na kizibao cha kuhani. 7 Saulo alipoambiwa kwamba Daudi amekwisha fika Keila, akasema: “Mungu amemutia katika mikono yangu maana amejifungia mwenyewe kwa kuingia katika muji wenye milango yenye vifungio.” 8 Kwa hiyo, Saulo aliwatuma waaskari waende Keila na kufanya mashambulizi, kwa kumukamata Daudi pamoja na watu wake. 9 Daudi aliposikia mipango miovu ya Saulo juu yake, akamwambia kuhani Abiatari: “Ulete hapa kile kizibao cha kuhani.” 10 Kisha Daudi akaomba: “Ee Yawe, Mungu wa Israeli, kwa hakika mimi mutumishi wako, nimesikia kwamba Saulo anapanga kuja kuangamiza muji wa Keila kwa sababu yangu. 11 Wakaaji wa Keila watanitia katika mikono ya Saulo? Saulo atakuja kweli kama nilivyosikia mimi mutumishi wako? Ee Yawe, Mungu wa Israeli, ninakuomba unijibu mimi mutumishi wako.” Yawe akamujibu: “Saulo atakuja.” 12 Daudi akamwuliza: “Wakaaji wa Keila watanitia katika mikono ya Saulo, mimi pamoja na watu wangu?” Yawe akamujibu: “Watakutia katika mikono yake.” 13 Kisha, Daudi na watu wake ambao walikuwa yapata mia sita, waliondoka na kwenda popote walipoweza kwenda. Saulo aliposikia kwamba Daudi amekwisha kimbia kutoka Keila, akaiacha mipango yake yote. Daudi katika inchi ya milima 14 Basi, Daudi alibaki katika makimbilio ndani ya jangwa, katika inchi ya milima ya mbuga za Zifu. Saulo alimutafuta kila siku, lakini Mungu hakumutia Daudi katika mikono yake. 15 Daudi alijua kwamba Saulo alitaka kuyaangamiza maisha yake. Daudi akabaki katika mbuga za Zifu, kule Horeshi. 16 Yonatani mwana wa Saulo akamufuata Daudi kule Horeshi, akamutia moyo kwamba Mungu anamulinda. 17 Yonatani akamwambia: “Usiogope, baba yangu Saulo hatakupata. Wewe utakuwa mufalme wa Israeli, mimi nitakuwa wa pili wako. Hata Saulo baba yangu anajua jambo hili.” 18 Hao wote wawili, wakafanya agano mbele ya Yawe. Daudi akabaki katika muji wa Horeshi na Yonatani akaenda zake kwenye nyumba. 19 Saulo alipokuwa angali kule Gibea, Wazifu wakamwendea na kumwambia: “Daudi anajificha katika inchi yetu kwenye makimbilio kule Horeshi, kwenye mulima Hakila, unaokuwa upande wa kusini wa jangwa. 20 Sasa, mufalme, ukuje kusudi utimize mambo yanayokuwa ndani ya moyo wako, na kwa upande wetu, kazi yetu itakuwa kumutia Daudi katika mikono yako.” 21 Saulo akawajibu: “Ninyi kweli munanionea huruma; Yawe awabariki. 22 Muende tena muhakikishe, mujue pahali anapojificha, na ni nani amemwona pahali pale; maana nimeambiwa kwamba yeye ni mwerevu sana. 23 Muchunguze kila upande mujue pahali anapojificha, kisha muniletee habari kamili. Halafu nitakwenda pamoja nanyi na ikiwa angali kule, basi, mimi nitamutafuta kati ya maelfu yote ya watu wa Yuda.” 24 Basi, wakaondoka kwenda Zifu, wakimutangulia Saulo. Wakati ule, Daudi na watu wake walikuwa katika mbuga za Maoni, katika bonde la Araba upande wa kusini wa jangwa. 25 Saulo na watu wake wakaanza kumutafuta Daudi. Lakini Daudi alipopata habari zile, alikwenda kujificha kwenye mawe makubwa, yanayokuwa katika mbuga za Maoni na kukaa kule. Saulo aliposikia habari zile, alimufuatilia Daudi kule kwenye mbuga za Maoni. 26 Saulo na watu wake walikuwa upande mumoja wa mulima, na Daudi na watu wake walikuwa upande mwingine wa mulima. Daudi alipokuwa anaharakisha kukimbia, Saulo naye alikuwa anamukaribia kwa kumukamata Daudi. 27 Hapo mutu mumoja akamwendea Saulo na kumwambia: “Kuja haraka; Wafilistini wanaishambulia inchi.” 28 Kwa hiyo, Saulo akaacha kumufuatilia Daudi, akaenda kupigana na Wafilistini. Ndiyo maana pahali pale pakaitwa “Jiwe la Matengano.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo