Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

1 Samweli 17 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Goliati anapambana na Waisraeli

1 Wafilistini walikusanya makundi yao ya waaskari kule Soko, muji unaokuwa katika inchi ya Yuda, tayari kwa vita. Walipiga kambi katika sehemu moja inayoitwa Efesi-Damimu kati ya Soko na Azeka.

2 Saulo pamoja na Waisraeli walikusanyika, na kupiga kambi katika bonde la Ela. Wakajipanga tayari kwa kupigana na Wafilistini.

3 Wafilistini walisimama kwenye mulima upande mumoja na Waisraeli walisimama kwenye mulima upande mwingine. Katikati yao kulikuwa bonde.

4 Kutoka kwenye kambi ya Wafilistini, shujaa mumoja anayeitwa Goliati, wa muji wa Gati, alijitokeza. Urefu wake ulikuwa metre tatu.

5 Kwenye kichwa chake alivaa kofia ya shaba, na nguo ya shaba kwa kifua yenye uzito wa kilo makumi tano na saba.

6 Miguu yake vilevile ilikuwa na vikingio vya shaba na kwenye mabega yake alibeba mukuki wa shaba.

7 Mupini wa mukuki wake ulikuwa kama muti wa mufumaji wa nguo, na chuma cha mukuki huo, kilikuwa na uzito wa kilo saba. Ngao yake ilibebwa na mutu mwingine aliyemutangulia.

8 Goliati alisimama na kuwapigia kelele waaskari wa Waisraeli, akisema: “Munafanya nini pale? Mumekuja kupigana vita? Mimi ni Mufilistini; ninyi ni watumwa wa Saulo. Muchague mutu mumoja kati yenu akuje kupigana nami.

9 Akinishinda na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu. Lakini nikimushinda na kumwua basi, ninyi mutakuwa watumwa wetu na kututumikia.”

10 Kisha Mufilistini yule aliendelea kusema kwa majivuno: “Ninawataka waaskari wa Waisraeli siku hii kumutoa mutu mumoja akuje kupigana nami.”

11 Saulo pamoja na waaskari wote wa Israeli walipoyasikia maneno hayo ya Mufilistini yule, walifazaika na kuogopa sana.


Daudi kwenye kambi ya Saulo

12 Daudi alikuwa mutoto wa Yese, wa ukoo wa Efurata kutoka Betelehemu katika inchi ya Yuda. Yese alikuwa na watoto wanane wa kiume. Wakati Saulo alipokuwa mufalme, yeye alikuwa amekwisha kuwa muzee, mutu mwenye umri mukubwa.

13 Wana wakubwa watatu wa Yese, Eliabu muzaliwa wa kwanza, Abinadabu aliyefuata na Shama wa tatu, walikuwa wamekwenda pamoja na Saulo kwenye vita.

14 Daudi alikuwa ndiye mudogo kati ya wote. Wale watoto watatu wakubwa walikuwa wamekwenda na Saulo.

15 Ingawa Daudi mara kwa mara alikwenda kwa Saulo, alirudi kwenda Betelehemu kuchunga kondoo wa baba yake.

16 Kwa muda wa siku makumi ine, asubui na magaribi, yule Mufilistini Goliati alijitokeza, akasimama na kuwazarau waaskari wa Waisraeli.

17 Siku moja, Yese alimwambia mwana wake Daudi: “Uwapelekee kaka zako kilo kumi za ngano yenye kukaangwa na mikate kumi. Uwapelekee haraka kule katika kambi.

18 Na yule mukubwa wa kundi la waaskari elfu moja umupelekee siagi hizi kumi. Uwaangalie kaka zako kama wanaendelea vizuri na kisha uniletee habari zao.”

19 Wakati ule, mufalme Saulo, kaka za Daudi na waaskari wote wa Israeli walikuwa kwenye bonde la Ela, wanapigana na Wafilistini.

20 Kesho yake, Daudi aliamuka asubui mapema, na akamwachia muchungaji mumoja kondoo. Alibeba chakula na kwenda kama vile alivyoagizwa na baba yake Yese. Alipofika kwenye kambi ya Waisraeli, aliwakuta wanajipanga kwenye sehemu yao ya vita na wanapiga kelele za vita.

21 Makundi ya waaskari ya Waisraeli na ya Wafilistini walijipanga tayari kupigana vita, makundi yakiwa yanaangaliana uso kwa uso.

22 Daudi alimupatia kile chakula mutu aliyechunga mizigo, akawakimbilia waaskari, akaenda kwa kaka zake na kuwasalimia.

23 Alipokuwa anaongea nao, Goliati, yule shujaa wa Wafilistini kutoka Gati, alijitokeza mbele ya waaskari wa Israeli kama vile alivyozoea. Naye Daudi alimusikiliza vizuri sana.

24 Waisraeli walipomwona Goliati, walimukimbia, na kumwogopa sana.

25 Waliambiana: “Mumemwona yule mutu aliyejitokeza? Yeye amejitokeza kwa kuwazarau Waisraeli. Mufalme Saulo atamupa mutu yeyote atakayemwua mutu yule utajiri mwingi. Zaidi ya yote, atamupatia vilevile binti yake kusudi amwoe. Tena, watu wa jamaa ya baba yake watakuwa huru, hawatalipa kodi.”

26 Daudi akawauliza wale waliokuwa karibu naye: “Mutu atakayemwua Mufilistini huyu na kuikomboa Israeli kutokana na haya hii atafanyiwa nini? Ni nani huyu Mufilistini, mutu mupagani, anayesubutu kuwatukana waaskari wa Mungu Mwenye Uzima?”

27 Watu wakamwambia kama walivyokuwa wamesema pale mbele juu ya mutu atakayemwua Goliati.

28 Lakini Eliabu, kaka mukubwa wa Daudi alipomusikia Daudi akiongea na watu, alimukasirikia Daudi, akasema: “Kwa nini umekuja? Wale kondoo wachache umemwachia nani kule katika mbuga? Ninajua majivuno yako na uovu wa moyo wako. Umekuja tu kutazama vita.”

29 Daudi akamujibu: “Sasa nimefanya nini? Siwezi kuuliza neno tu?”

30 Daudi akamugeukia mutu mwingine, akamwuliza neno lilelile; na kila mara alipouliza, alipata jibu lilelile.

31 Watu fulani ambao walimusikia Daudi alivyosema, walikwenda kumwambia Saulo. Naye Saulo akaagiza aitwe.

32 Daudi akamwambia Saulo: “Mutu yeyote asitishike ndani ya moyo wake kutokana na Mufilistini huyu. Mimi mutumishi wako nitakwenda kupigana naye.”

33 Saulo akamwambia Daudi: “Wewe hauwezi kwenda kupigana na Mufilistini yule. Wewe ni kijana tu, lakini mutu yule amekuwa katika vita tangu ujana wake.”

34 Daudi akasema: “Mimi mutumishi wako nimezoea kuchunga kondoo wa baba yangu. Kila wakati simba au dubu akikuja na kukamata mwana-kondoo

35 mimi ninamufuata na kumushambulia, nikimwokoa mwana-kondoo toka katika kinywa chake. Kama simba au dubu akinishambulia, mimi ninamushika ndevu zake, nikimwangusha na kumwua.

36 Mimi mutumishi wako nimekwisha kuua simba wengi na dubu wengi. Sasa, hata yule Mufilistini mupagani, ambaye amewatukana waaskari wa Mungu Mwenye Uzima, atakuwa kama wao.

37 Yawe ambaye ameniokoa toka katika makucha ya simba na dubu, ataniokoa kutoka kwa Mufilistini huyu.” Saulo akamwambia: “Kwenda, naye Yawe akuwe pamoja nawe.”

38 Saulo akamuvalisha Daudi nguo zake za kivita, akamuvalisha kofia yake ya shaba juu ya kichwa na koti lake la kifua.

39 Daudi akajifunga upanga wa Saulo, akajaribu kutembea; lakini akashindwa kwa sababu hakuzoea nguo kama hizo. Akamwambia Saulo: “Siwezi kwenda katika vita nikiwa nimevaa nguo hizi, maana mimi sijazizoea.” Kwa hiyo, akazivua.

40 Daudi akatwaa fimbo yake katika mukono, akajichagulia mawe matano mazuri kutoka kwenye kijito, akayatia katika mufuko wake wa muchungaji. Mujeledi wake ulikuwa tayari katika mukono wake, akaanza kumwendea Goliati Mufilistini.


Daudi anamushinda Goliati

41 Yule Mufilistini, naye akaanza kumwendea Daudi, na yule aliyemubebea ngao yake akiwa mbele yake.

42 Yule Mifilistini alipoangalia na kumwona vizuri Daudi, alimuzarau, maana Daudi alikuwa kijana muzuri mwenye afya nzuri na wa kupendeza.

43 Goliati akamwuliza Daudi: “Sasa, hiyo fimbo ni ya nini? Unazani mimi ni imbwa hata unifikie kwa fimbo?” Mufilistini yule akamulaani Daudi kwa miungu yake.

44 Mufilistini akamwambia Daudi: “Kuja kwangu! Mwili wako nitawapa ndege na nyama wa pori!”

45 Lakini Daudi akamwambia Goliati: “Wewe unanifikia kwa upanga na mikuki. Lakini mimi ninakufikia kwa jina la Yawe wa majeshi, Mungu wa waaskari wa Israeli, ambaye wewe umemutukana.

46 Siku ya leo, Yawe atakutia katika mikono yangu. Nitakushinda, nitakukata kichwa chako; na miili ya waaskari wa Wafilistini nitawapa ndege na nyama wa pori. Halafu dunia nzima itajua kwamba Mungu yuko katika Israeli.

47 Watu wote waliokusanyika hapa leo, watajua kwamba Yawe hahitaji mikuki kwa kuwaokoa watu. Hii ni vita ya Yawe, naye atawatia ninyi wote katika mikono yetu.”

48 Goliati akaanza tena kumwendea Daudi. Daudi akakimbia mbio kwenda kwenye mustari wa mapambano.

49 Akatia mukono wake ndani ya mufuko wake, akatoa jiwe moja, akalirusha kwa mujeledi wake, akamupiga nalo Goliati kwenye paji la uso wake, jiwe likalipasua paji la Goliati na kupenya ndani. Goliati akaanguka uso mpaka chini.

50 Ndivyo Daudi alivyomushinda Goliati kwa mujeledi wake na jiwe. Alimupiga yule Mufilistini na kumwua. Daudi hakukuwa na upanga wowote katika mukono wake.

51 Basi, akaenda mbio, akasimama juu ya Goliati, akachomoa upanga wa Goliati toka katika mufuko wake, akamwua Goliati kwa kumukata kichwa chake. Wafilistini walipoona kwamba shujaa wao ameuawa, wakakimbia mbio.

52 Halafu watu wa Israeli na watu wa Yuda walianza kupiga kelele za ushindi, wakawafuatilia Wafilistini mpaka Gati, kwenye milango ya muji wa Ekroni, hata Wafilistini walioumizwa katika vita walikufa katika njia tangu Saraimu mpaka Gati na Ekroni.

53 Waisraeli walipotoka kuwafuatilia Wafilistini, waliteka vitu ndani ya kambi yao.

54 Daudi alikitwaa kichwa cha yule Goliati Mufilistini, akakipeleka katika muji wa Yerusalema. Lakini silaha za Goliati akaziweka katika hema yake.


Daudi anapelekwa kwa Saulo

55 Saulo alipomwona Daudi akienda kupigana na yule Mufilistini Goliati, alimwuliza Abeneri, jemadari wa kundi lake: “Abeneri, huyu ni kijana wa nani?” Abeneri alijibu: “Ee Mufalme, ninaapa kwa jina lako, mimi sijui.”

56 Mufalme Saulo akamwambia: “Basi, uliza yeye ni kijana wa nani.”

57 Mara tu Daudi aliporudi katika kambi nyuma ya kumwua Goliati, Abeneri alimukamata na kumupeleka kwa Saulo. Wakati ule Daudi alikuwa angali akibeba kichwa cha Goliati katika mikono yake.

58 Saulo akamwuliza Daudi: “Kijana, wewe ni mwana wa nani?” Daudi akajibu: “Mimi ni mwana wa mutumishi wako Yese, kutoka muji wa Betelehemu.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan