Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

1 Samweli 14 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Kitendo cha uhodari cha Yonatani

1 Siku moja, Yonatani mwana wa mufalme Saulo alimwambia kijana aliyemubebea silaha: “Kuja, tuende ngambo kwenye kambi ya Wafilistini.” Lakini Yonatani hakumwambia baba yake.

2 Saulo alikuwa amepiga kambi chini ya muti wa mukomamanga kule Migroni, inje ya muji wa Gibea, akiwa pamoja na watu yapata mia sita.

3 Ahiya mwana wa Ahitubu ndugu yake na Ikabodi mwana wa Finehasi mujukuu wa Eli kuhani wa Yawe katika muji wa Shilo, alikuwa ndiye aliyevaa kizibao cha kuhani. Watu hawakujua kwamba Yonatani amekwisha ondoka.

4 Kwenye mapito ya mulima ambako Yonatani alipaswa kuvukia kusudi afike kwenye kambi ya Wafilistini, kulikuwa chongo mbili, upande mumoja na upande mwingine. Chongo moja iliitwa Bozezi na ingine iliitwa Sene.

5 Chongo moja ilikuwa upande wa kaskazini wa muji wa Mikimasi na ingine ilikuwa upande wa kusini kuelekea muji wa Gibea.

6 Yonatani akamwambia yule kijana aliyemubebea silaha: “Kuja, tuende kwenye ile kambi ya hawa watu wasiotahiriwa. Labda Yawe atatusaidia, maana Yawe haokoi kwa kutegemea wingi au uchache wa watu.”

7 Yule kijana aliyemubebea silaha akamwambia: “Fanya chochote unachotaka kufanya, mimi niko pamoja nawe maana wazo lako ndilo wazo langu.”

8 Yonatani akamwambia: “Tutavuka kuwaendea wale watu kusudi wapate kutuona.

9 Kama wakituambia tuwangojee mpaka wafike hapa tunapokuwa, basi, tutasimama hapa hapa wala hatutawaendea.

10 Lakini wakisema sisi tuwaendee, basi tutawaendea maana hicho kitakuwa ni kitambulisho kwamba Yawe amewatia katika mikono yetu.”

11 Basi, wakajitokeza kusudi Wafilistini wawaone. Wafilistini walipowaona wakasema: “Muangalie wale Waebrania wanatoka kwenye mashimo walimokuwa wamejificha.”

12 Wafilistini waliokuwa kwenye kambi wakamwita Yonatani na kijana aliyemubebea silaha: “Mukuje huku kwetu, nasi tutawaonyesha kitu.” Yonatani akamwambia yule kijana aliyemubebea silaha: “Unifuate. Yawe amewatia katika mikono ya Waisraeli.”

13 Basi, Yonatani akapanda akitembea kwa miguu na mikono, na yule kijana akamufuata. Yonatani aliwashambulia Wafilistini akiwaangusha chini na yule kijana alifuata nyuma akiwaua.

14 Katika mashambulizi hayo ya kwanza, Yonatani akiwa pamoja na kijana wake aliyemubebea silaha, aliwaua watu yapata makumi mbili katika eneo kidogo tu.

15 Kulikuwa hofu kubwa katika kambi ya Wafilistini. Wote walianza kufazaika: waaskari katika kambi, watu katika mashamba kwenye kambi, hata na washambulizi. Inchi ilitetemeka. Hofu ilikuwa kubwa sana.


Kushindwa kwa Wafilistini

16 Wapelelezi wa Saulo kule Gibea katika inchi ya Benjamina waliwaona watu wengi wakikimbia huku na huko.

17 Saulo akawaambia watu waliokuwa pamoja naye: “Basi mujihesabu kwa kujua ni nani waliotutoroka.” Walipojihesabu, waligundua kwamba Yonatani na kijana aliyemubebea silaha walikuwa hawapo.

18 Saulo akamwambia kuhani Ahiya: “Ulete hapa Sanduku la Agano la Mungu.” (Wakati huo Sanduku la Agano la Mungu lilikuwa pamoja na Waisraeli.)

19 Saulo alipokuwa angali anaongea na kuhani, fujo katika kambi ya Wafilistini iliongezeka zaidi na zaidi. Kwa hiyo Saulo akamwambia kuhani: “Acha. Usililete tena Sanduku la Agano.”

20 Hivyo, Saulo na watu wake wakajipanga na kuingia katika vita na Wafilistini. Lakini Wafilistini walianza kushambuliana wenyewe kwa wenyewe kwa muvurugiko mukubwa.

21 Waebrania waliokuwa upande wa Wafilistini, na waliokwenda nao kule katika kambi, wakageuka na kujiunga na Waisraeli waliokuwa pamoja na Saulo na Yonatani.

22 Hata Waisraeli wengine waliokuwa wamejificha kwenye inchi ya milima ya Efuraimu, waliposikia kwamba Wafilistini walikuwa wanakimbia, nao vilevile wakawafuatilia na kuwapiga.

23 Hivyo Yawe aliwapa Waisraeli ushindi. Vita ilienea mpaka kupita Beti-Aweni.


Matukio nyuma ya vita

24 Siku ile, Waisraeli walisumbuliwa sana maana Saulo alikuwa amewaapiza watu akisema: “Alaaniwe mutu yeyote atakayekula chakula mbele jua kutua, na mbele sijajilipiza waadui zangu kisasi.” Kwa hiyo, siku yote, hakuna mutu aliyeonja chakula chochote.

25 Watu wote walipofika katika pori, walikuta asali iliyosambaa hata chini kwenye udongo.

26 Ingawa watu walipofika katika pori na kukuta asali ikidondoka kila nafasi, hakuna mutu aliyesubutu kula asali hiyo kwa kuogopa kile kiapo walichoapishwa.

27 Lakini Yonatani hakusikia wakati baba yake alipowaapiza watu. Halafu akainua fimbo aliyokuwa nayo, akaichovya kwenye sega la asali, akakula asali hiyo. Hapo akajisikia kuwa na nguvu.

28 Mutu mumoja akamwambia: “Baba yako aliwaapiza watu vikali, akisema: ‘Mutu yeyote atakayekula chakula leo alaaniwe.’ ” Nao watu walikuwa wazaifu kwa ajili ya njaa.

29 Yonatani akajibu: “Baba yangu anawasumbua watu. Sasa mimi ninajisikia kuwa na nguvu kwa sababu nimeonja asali hii kidogo.

30 Kama tu waaskari wetu wangeweza kula kidogo kutoka vitu walivyoteka kutoka kwa waadui zao, wengi zaidi kati ya Wafilistini wangaliuawa.”

31 Siku ile, Waisraeli waliwapiga Wafilistini, tangu Mikimasi mpaka Ayaloni. Wakati huu Waisraeli walikuwa wamechoka kwa sababu ya njaa.

32 Basi walikimbilia vitu walivyoteka, wakatwaa wana-kondoo, ngombe dume na wana-ngombe, wakachinja, wakakula nyama na damu.

33 Watu wengine wakamwambia Saulo: “Angalia watu wanatenda zambi mbele ya Yawe kwa kula nyama yenye damu.” Saulo akawaambia watu: “Ninyi ni waasi. Muviringishe jiwe kubwa na kulileta hapa.”

34 Akawaambia: “Muende muwaambie watu wote walete ngombe na kondoo wao hapa, wawachinje na kuwakula hapa. Wasitende zambi mbele ya Yawe, kwa kula nyama yenye damu.” Hivyo, usiku ule wote walipeleka ngombe wao na kuwachinjia pale.

35 Saulo akamujengea Yawe mazabahu. Hiyo ilikuwa ndiyo mazabahu ya kwanza ambayo Saulo alimujengea Yawe.

36 Kisha Saulo akawaambia watu: “Twende tuwafuatilie Wafilistini usiku, tuwashambulie na kunyanganya mali zao mpaka asubui. Hatutamwacha mutu yeyote muzima.” Watu wakamwambia: “Fanya unachoona kuwa chema kwako.” Lakini kuhani akawaambia: “Kwanza tuombe shauri kwa Yawe.”

37 Hivyo, Saulo akamwuliza Mungu: “Niende kuwashambulia Wafilistini? Utawatia katika mikono ya Waisraeli?” Lakini Mungu hakujibu kitu siku hiyo.

38 Saulo akasema: “Mukuje hapa enyi viongozi wa watu, tujue ni zambi gani tumetenda leo.

39 Kama vile Yawe Mwokozi wa Israeli anavyoishi, hata kama ni mwana wangu Yonatani anapaswa kuuawa.” Lakini hakuna mutu aliyesema neno.

40 Kwa hiyo, Saulo akawaambia: “Ninyi wote musimame upande ule, halafu mimi na mwana wangu Yonatani tutasimama upande huu.” Wao wakajibu: “Fanya chochote unachoona kinafaa.”

41 Saulo akasema: “Ee Yawe wa Israeli, kwa nini haujanijibu mimi mutumishi wako? Ee Yawe wa Israeli, ikiwa kosa liko kwangu au kwa Yonatani mwana wangu, basi, jiwe la Urimu lionekane. Lakini ikiwa kosa hilo liko kwa watu wako Waisraeli, jiwe la Tumimu lionekane.” Yonatani na Saulo walipatikana kuwa na kosa, lakini watu walionekana hawana kosa.

42 Saulo akasema: “Mupige kura kati yangu na mwana wangu Yonatani.” Yonatani akapatikana kuwa na kosa.

43 Kwa hiyo Saulo akamwambia Yonatani: “Uniambie jambo ulilofanya.” Yonatani akajibu: “Nilikula asali kidogo kwa kutumia fimbo yangu. Niko hapa na niko tayari kufa.”

44 Saulo akasema: “Mungu aniue ikiwa Yonatani hatauawa.”

45 Lakini watu wakamwambia Saulo: “Kwa nini Yonatani, aliyeletea Waisraeli ushindi huu mukubwa, auawe? Haiwezikani hata kidogo. Kama vile Yawe anavyoishi, hata unywele mumoja wa kichwa chake hautaanguka chini. Alichokifanya leo, amekifanya kwa musaada wa Yawe.” Kwa hiyo, watu walimukomboa Yonatani naye hakuuawa.

46 Kisha Saulo aliacha kuwafuatilia Wafilistini, nao Wafilistini wakarudi kwao.


Utawala wa Saulo na jamaa yake

47 Saulo alipokwisha kuwa mufalme wa Waisraeli, alipigana na waadui zake wote kila upande: Wamoabu, Waamoni, Waedomu, wafalme wa Zoba na Wafilistini. Kila mara alipopigana vita, alishinda.

48 Alipigana kwa uhodari, akawashinda Waamaleki. Aliwaokoa Waisraeli kutokana na watu wote waliowashambulia.

49 Wana wa Saulo walikuwa: Yonatani, Iswi na Malkisua. Wabinti zake walikuwa wawili; muzaliwa wa kwanza aliitwa Merabu na mudogo aliitwa Mikali.

50 Muke wa Saulo aliitwa Ahinoamu binti ya Ahimasi. Jemadari wa makundi ya waaskari wa Saulo aliitwa Abeneri mwana wa Neri, baba mudogo wa Saulo.

51 Baba wa Saulo aliitwa Kisi na baba wa Abeneri aliitwa Neri mwana wa Abieli.

52 Kulikuwa vita kali na Wafilistini kwa muda wote Saulo alipokuwa mufalme. Na kila mara Saulo alipomupata mutu mwenye nguvu au shujaa alimukamata apate kujiunga na waaskari wake.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan