Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

1 Samweli 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Elekana na jamaa yake kule Shilo

1 Kulikuwa mutu mumoja katika muji wa Rama katika inchi ya milima ya Efuraimu jina lake Elekana wa kabila la Efuraimu. Yeye alikuwa mwana wa Yerohamu, na mujukuu wa Elihu mwana wa Tohu mwana wa Zufu.

2 Elekana alikuwa na wake wawili, mumoja aliitwa Hana na wa pili Penina. Penina alikuwa na watoto, lakini Hana hakukuwa na watoto.

3 Kila mwaka Elekana alisafiri kutoka Rama kwenda kuabudu na kumutolea Yawe wa majeshi sadaka kule Shilo. Kule, wana wawili wa Eli, Hofuni na Finehasi, walikuwa makuhani wa Yawe.

4 Kila wakati Elekana alipotoa sadaka alimupa muke wake Penina fungu moja la nyama ya sadaka na fungu mojamoja kwa watoto wake wa kiume na wa kike.

5 Elekana alimupa Hana fungu kubwa la nyama ya sadaka kwa sababu alimupenda sana ingawa Yawe hakumujalia watoto.

6 Penina alikuwa akimuchokoza sana Hana kusudi amukasirikishe kwa sababu Yawe hakumujalia Hana watoto.

7 Mambo hayo yaliendelea kila mwaka. Kila mara Hana alipokwenda kwenye nyumba ya Yawe, Penina alimukasirikisha Hana hata Hana akalia na kukataa kula chochote.

8 Mume wake Elekana alimwuliza: “Kwa nini unalia? Kwa nini hautaki kula? Kwa nini una huzuni ndani ya moyo wako? Basi, mimi si bora kwako kuliko watoto kumi wa kiume?”


Hana na Eli

9 Siku moja, walipokuwa wamemaliza kula na kunywa katika nyumba ya Yawe kule Shilo, Hana akasimama. Wakati ule, kuhani Eli alikuwa ameikaa kwenye kiti karibu na mulango wa nyumba ya Yawe.

10 Hana alikuwa na huzuni sana. Na alipokuwa anamwomba Yawe akakuwa analia kwa uchungu.

11 Akafanya kiapo akisema: “Ee Yawe wa majeshi, kama tu utayaangalia mateso yangu mimi mujakazi wako, ukinikumbuka mimi, bila kunisahau, mimi mujakazi wako, ukinijalia mimi mujakazi wako mutoto mwanaume, nitakupa wewe Yawe mutoto huyo akuwe wako maisha yake yote; wembe hautapita kwenye kichwa chake hata kidogo.”

12 Hana aliendelea kumwomba Yawe kwa muda murefu, na kuhani Eli akakuwa anaangalia midomo yake.

13 Hana alikuwa akiomba kimoyomoyo, midomo yake ilikuwa inachezacheza, lakini sauti yake haikusikilika. Hivyo Eli akafikiri kwamba Hana amelewa.

14 Kwa hiyo Eli akamwambia: “Utaendelea kulewa mpaka wakati gani? Achana na kunywa divai.”

15 Lakini Hana akamujibu: “Sivyo bwana wangu. Mimi ni mwanamuke mwenye taabu sana; mimi sijakunywa divai wala kinywaji kikali, lakini nimekuwa nikimutolea Yawe yanayokuwa ndani ya roho yangu.

16 Usinizanie kuwa mimi ni mwanamuke asiyefaa kitu. Kwa muda wote huu nimekuwa nikisema mahangaiko yangu na taabu yangu.”

17 Halafu Eli akamwambia: “Kwenda kwa amani; naye Mungu wa Israeli akupe kile ulichomwomba.”

18 Hana akasema: “Ninaomba nami mujakazi wako nipate kukubaliwa mbele yako.” Hana akaenda zake, akakula chakula na hakukuwa na huzuni tena.


Kuzaliwa kwa Samweli

19 Kesho yake asubui, Elekana na jamaa yake waliamuka asubui mapema, na kisha kumwabudu Yawe, walirudi kwao Rama. Elekana akalala na muke wake Hana na Yawe akamukumbuka.

20 Hivyo Hana akapata mimba, akazaa mutoto wa kiume. Hana akamwita mutoto huyo Samweli, maana alisema: “Nimemwomba kwa Yawe.”

21 Elekana na jamaa yake yote wakaenda tena Shilo na kumutolea Yawe sadaka ya kila mwaka na kutimiza kiapo.

22 Lakini mara hii Hana hakuenda, maana alimwambia mume wake hivi: “Mara tu mutoto atakapoachishwa kunyonya, nitamupeleka kusudi awekwe mbele ya Yawe, abakie kule siku zote.”

23 Mume wake Elekana, akamujibu: “Fanya unaloona linafaa. Ngojea mpaka utakapomwachisha mutoto kunyonya. Yawe afanye kiapo chako kuwa kweli.” Basi, Hana alibaki kwake, akaendelea kumulea mutoto wake mpaka alipomwachisha kunyonya.

24 Alipomwachisha kunyonya alimupeleka pamoja na ngombe dume wa miaka mitatu, gunia la unga na karabia ya divai. Hana alimwingiza mutoto kwenye nyumba ya Yawe kule Shilo, naye mutoto alikuwa mudogo tu.

25 Walipokwisha kuchinja yule ngombe dume, walimupeleka mutoto kwa kuhani Eli.

26 Hana akamwambia: “Ee bwana wangu, kama vile unavyoishi, bwana wangu, mimi ni yule mwanamuke aliyekuwa anasimama mbele yako akimwomba Yawe.

27 Nilimwomba anipe mutoto huyu, na yeye alinipa kile nilichomwomba.

28 Kwa sababu hiyo, mimi ninamupa Yawe mutoto huyu; wakati wote atakapokuwa anaishi, ametolewa kwa Yawe.” Halafu, wakamwabudu Yawe pale.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan