1 Petro 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maonyo kwa wazee wa kanisa 1 Ninawaonya wazee wa kanisa wanaokuwa kati yenu. Mimi vilevile ni muzee mwenzenu, nami ni mushuhuda wa mateso ya Kristo na zaidi ya hii nitashiriki katika utukufu ule utakaotokea. 2 Ninawaonya, muchunge lile kundi Mungu alilowapatia, si kwa kulazimishwa, lakini kwa mapenzi yenu sawa vile Mungu anavyotaka. Musitumike kwa ajili ya tamaa mbaya ya mali, lakini kwa kujitoa kwa moyo mwema. 3 Musitawale kwa kinguvu kundi lile lililowekwa chini ya uangalizi wenu, lakini mukuwe mifano kwao. 4 Na wakati Muchungaji Mukubwa atakapotokea, mutapokea taji ya utukufu isiyoweza kuharibika. 5 Na hivi vilevile, ninyi vijana, munapaswa kuwatii hao wazee. Ninyi wote munapaswa kuwa na unyenyekevu, mupate kutumikiana; maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Mungu anawapinga wenye kiburi, lakini anawajalia wanyenyekevu neema.” 6 Basi mujinyenyekeze mbele ya Mungu mwenye uwezo, kusudi awainue kwa wakati unaofaa. 7 Mumutolee masumbuko yenu yote kwa maana yeye anawashugulikia. 8 Mukuwe waangalifu na mukeshe, kwa maana adui yenu Shetani anazungukazunguka kama simba anayenguruma akitafuta yule atakayerarua. 9 Mupingane naye, mukisimama imara katika imani, mukijua kwamba fasi zote katika dunia, wandugu zenu wanapata mateso kama hayo. 10 Lakini mukisha kuteswa kwa muda kidogo, Mungu mwenye neema yote aliyewaita kusudi mupate kushiriki naye katika utukufu wake wa milele katika kuungana kwenu na Kristo, yeye mwenyewe atawakamilisha. Atawatia nguvu na kuwasimamisha imara kabisa. 11 Yeye ndiye Mungu mwenye uwezo kwa milele na milele. Amina. Salamu za mwisho 12 Nimewaandikia barua hii fupi nikisaidiwa na Sila, ninayemujua kuwa ndugu mwaminifu. Ninataka kuwatia moyo na kushuhudia kwenu kwamba mambo hayo yanayoelekea neema ya Mungu ni ya kweli; nanyi musikose kushikamana nayo. 13 Kanisa linalokuwa katika Babeli, lililochaguliwa na Mungu kama vile ninyi, linawasalimia. Vilevile Marko, mwana wangu katika imani, anawasalimia. 14 Musalimiane kwa upendo wa kindugu. Ninawatakia amani ninyi watu wote wa Kristo. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo