1 Mambo ya Siku 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Sanduku la Agano linasimamishwa Kiriati-Yearimu ( 2 Sam 6.1-11 ) 1 Daudi akashauriana na majemadari wa makundi ya maelfu na makundi ya mamia, pamoja na viongozi wote. 2 Kisha akawaambia Waisraeli wote waliokusanyika: “Ikiwa mutakubaliana nami, na ikiwa ni mapenzi ya Yawe, Mungu wetu, tufanye hivi: tutume wajumbe waende wawaite wandugu zetu waliobaki katika inchi ya Israeli, pamoja na makuhani na Walawi wanaokuwa katika miji yao na mashamba ya malisho yao, wakuje kukusanyika pamoja nasi. 3 Kisha tuende tukamate Sanduku la Agano la Mungu wetu, maana hatukulijali wakati wa utawala wa mufalme Saulo.” 4 Watu wote wakakubaliana na pendekezo lile maana waliliona kuwa jambo jema. 5 Kwa hiyo, Daudi akawakusanya Waisraeli wote katika inchi, tokea kwenye kijito cha Sihori kinachokuwa Misri, mpaka kwenye kiingilio cha Hamati kwa kulileta Sanduku la Agano toka Kiriati-Yearimu. 6 Daudi akiandamana na Waisraeli wote, akaenda mpaka katika muji wa Bala, ni kusema Kiriati-Yearimu, katika inchi ya Yudea, kwa kulitwaa toka kule Sanduku la Agano linaloitwa kwa jina la Yawe anayeikaa kwenye kiti chake cha kifalme juu ya makerubi. 7 Basi, wakalitwaa Sanduku la Agano kutoka katika nyumba ya Abinadabu wakilibeba juu ya gari jipya. Uza na Ahio wakaongoza gari lile. 8 Daudi na Waisraeli wote wakakuwa wanacheza kwa nguvu zao zote, mbele ya Mungu. Waliimba nao wakikuwa wanapiga ala za muziki zilizotengenezwa kwa muti wa muvinje: vinubi, vinanda, matari, matoazi na baragumu. 9 Walipofika kwenye uwanja wa kupepetea ngano wa Kidoni, Uza akaunyoosha mukono wake kwa kuzuia Sanduku la Agano kwa sababu ngombe walijikwaa. 10 Mara moja Yawe akamukasirikia Uza kwa kuligusa sanduku, akamwua. Uza akakufa palepale mbele ya Mungu. 11 Daudi akakasirika kwa sababu Yawe alimwua Uza akiwa na hasira. Kwa sababu hiyo, pahali pale panaitwa Pigo la Uza mpaka leo. 12 Siku hiyo Daudi akamwogopa Mungu, akasema: “Sasa, nitaweza namna gani kupeleka Sanduku la Agano katika nyumba yangu?” 13 Basi, Daudi hakupeleka sanduku mpaka katika muji wa Daudi, lakini akalipeleka katika nyumba ya Obedi-Edomu wa Gati. 14 Sanduku lile la Mungu lilikaa kule kwa Obedi-Edomu kwa muda wa miezi mitatu, naye Yawe akabariki nyumba ya Obedi-Edomu na mali yake yote. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo