Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

1 Mambo ya Siku 12 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Wasaidizi wa kwanza wa Daudi wa kabila la Benjamina

1 Hawa ndio wanaume ambao walijiunga na Daudi kule Ziklagi, alipokuwa hana uhuru wowote wa kutembea kwa sababu ya mufalme Saulo mwana wa Kisi. Watu hawa walikuwa kati ya waaskari mashujaa waliomusaidia katika vita.

2 Walikuwa wa kabila la Benjamina kama vile Saulo alivyokuwa. Walikuwa wapiga upinde hodari, na warusha mawe hodari kwa kutumia mikono yote, wa kuume na wa kushoto. Haya ndiyo majina yao:

3-8 Kiongozi wao alikuwa Ahiezeri aliyesaidiwa na Yoasi, wote wawili ni wana wa Sema kutoka Gibea, Yezieli na Peleti, wana wa Azimaweti, Beraka na Yehu kutoka Anatoti, Isimaya kutoka Gibeoni aliyekuwa mutu shujaa kati ya wale makumi tatu na kiongozi wao, Yeremia, Yahazieli, Yohanani, Yozabadi kutoka Gedera, Elizai, Yeremoti, Bealia, Semaria, na Sefatia wa muji wa Harufi, Elekana, Isia, Azareli, Yoezeri, Yasobeamu kutoka ukoo wa Kora, Yoela na Zebadia, wana wa Yerohamu, kutoka Gedori.

9-14 Kutoka kabila la Gadi, hawa ndio waaskari mashujaa na walioelewa sana vita. Wakatoka kwao kwenda kujiunga na kundi la Daudi alipokuwa katika maficho kule katika jangwa. Walikuwa hodari wa kutumia mikuki na ngao, wenye nyuso za kuogopesha kama za simba, na katika milima walikuwa wepesi wa kukimbia kama swala. Kiongozi wao mukubwa alikuwa Ezeri. Alifuatwa na: Obadia, Eliabu, Misimana, Yeremia, Atai, Elieli, Yohana, Elisabadi, Yeremia, Makibanai.

15 Hao watu wa kabila la Gadi walikuwa wakubwa wa waaskari. Kulingana na vyeo vyao, mudogo alisimamia kundi la waaskari mia moja, na mukubwa alisimamia kundi la waaskari elfu moja.

16 Hawa ndio watu waliovuka muto Yordani katika mwezi wa kwanza, muto ulipokuwa umefurika pande zote na kuwatawanya watu kwa upande wa mashariki na magaribi ya muto.


Wasaidizi wa Daudi wa kabila la Benjamina na Yuda

17 Watu wamoja wa makabila ya Benjamina na Yuda wakafika pahali Daudi alipokuwa akijificha.

18 Daudi akatoka inje kwa kuwapokea, akawaambia: “Ikiwa mumekuja kwangu kama warafiki kwa kunisaidia basi ninawapokea kwa moyo wote, lakini kama mumekuja kwa kunitoa kwa waadui zangu, ingawa sijatenda ovu lolote, Mungu wa babu zetu awaone na kuwaazibu ninyi.”

19 Halafu Roho akamujaza Amasai, mukubwa wa wale watu makumi tatu, naye akasema: “Sisi ni watu wako, ee Daudi! Tuko upande wako, ee mwana wa Yese! Amani, amani ikuwe kwako, na amani ikuwe kwa yeyote anayekusaidia! Maana Mungu wako ndiye anayekusaidia.” Kisha Daudi akawapokea na kuwafanya wakubwa katika kundi lake.


Wasaidizi wa Daudi wa kabila la Manase

20 Waaskari wengine wa kabila la Manase, wakatoroka na kwenda kujiunga na Daudi, wakati alipoondoka pamoja na Wafilistini kwenda kupigana na mufalme Saulo. (Lakini hata hivyo, hakuwasaidia maana watawala wa Wafilistini walifanya shauri wamufukuze arudie Ziklagi wakisema: “Tutahatarisa maisha yetu kwa sababu atatutoroka na kurudia kwa bwana wake Saulo.”)

21 Basi, Daudi alipokuwa Ziklagi, watu hawa wa kabila la Manase wakamwendea: Adina, Yozabadi, Yediaeli, Mikaeli, Yozabadi, Elihu na Siletayi. Kila mumoja wao alikuwa kiongozi wa kundi la watu elfu moja katika kabila la Manase.

22 Wakamusaidia Daudi kupigana na makundi ya washambulizi, maana wote walikuwa waaskari mashujaa na majemadari wa waaskari.

23 Siku kwa siku, watu walijiunga na Daudi kwa kumusaidia, na nyuma akakuwa na kundi kubwa sana la waaskari, kama jeshi la Mungu.


Hesabu ya majeshi ya Daudi

24 Hii ndiyo hesabu ya makundi ya waaskari wenye silaha waliojiunga na Daudi kule Hebroni kwa kumutwalia ufalme kutoka kwa Saulo, kulingana na neno la Yawe:

25 Watu wa kabila la Yuda waliokuwa na mikuki na ngao, walikuwa elfu sita na mia nane. Wote walikuwa na silaha zao.

26 Kutoka kabila la Simeoni, watu elfu saba na mia moja mashujaa na wenye ujuzi mwingi wa vita.

27 Kutoka kabila la Lawi: watu elfu ine na mia sita.

28 Yehoyada, wa uzao wa Haruni na wenzake: watu elfu tatu na mia saba.

29 Jamaa za Zadoki, kijana hodari katika vita, yeye pamoja na majemadari makumi mbili na wawili kutoka ukoo wa baba yake mwenyewe.

30 Kutoka kabila la Benjamina, (kabila la Saulo): watu elfu tatu. Wengi wao walibaki waaminifu kwa jamaa ya Saulo.

31 Kutoka kabila la Efuraimu: watu elfu makumi mbili na mia nane, watu mashujaa sana tena waliheshimiwa katika ukoo zao.

32 Kutoka nusu ya kabila la Manase: watu elfu kumi na nane, waliotajwa majina kwa kuja kumuweka Daudi kuwa mufalme.

33 Kutoka kabila la Isakari: wakubwa mia mbili pamoja na wandugu zao wote waliokuwa chini ya waangozi wao. Wakubwa hao walikuwa na elimu ya kujua mambo ya nyakati na walijua mambo Waisraeli waliyopasha kufanya.

34 Kutoka kabila la Zebuluni: watu elfu makumi tano; waaminifu na wanaoelewa wa vita. Wakajitayarisha na silaha za vita za kila namna, shabaha yao ilikuwa ni kumusaidia Daudi tu.

35 Kutoka kabila la Nafutali: majemadari elfu moja pamoja na watu elfu makumi tatu na saba wenye ngao na mikuki.

36 Kutoka kabila la Dani: watu elfu makumi mbili na nane mia sita wenye silaha tayari kwa vita.

37 Kutoka kabila la Aseri: watu elfu makumi ine wenye kuelewa vita, tayari kwa mapigano.

38 Kutoka kabila la Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase kutoka ngambo ya muto Yordani: watu elfu mia moja na makumi mbili wenye kila aina ya silaha za vita.

39 Waaskari hao wote, waliojitayarisha kabisa kwa vita, walikwenda Hebroni na nia yao kubwa ikiwa ni kumuweka Daudi kuwa mufalme wa inchi yote ya Israeli. Nao watu wote wa Israeli, wakaungana wakiwa na nia moja ya kumuweka Daudi kuwa mufalme.

40 Basi, walikaa na Daudi kwa muda wa siku tatu, wakikula na kunywa maana wandugu zao walikuwa wamekwisha kuwatayarishia vyakula.

41 Zaidi ya hayo, wajirani zao wa karibu na hata wa mbali kama kule Isakari, Zebuluni na Nafutali, waliwaletea vyakula walivyobeba juu ya punda, ngamia, nyumbu na ngombe. Waliwaletea unga, mikate ya tini, zabibu zenye kukauka, divai na mafuta, ngombe na kondoo wengi, kukakuwa vyakula tele, maana kulikuwa furaha katika inchi ya Israeli.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan