Yoshua 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yoshua anawatuma wapelelezi Yeriko 1 Basi, Yoshua mwana wa Nuni, akawatuma watu wawili kwa siri kutoka Sitimu waende kufanya upelelezi katika inchi ile na hasa muji wa Yeriko. Wakaenda, wakafika kwenye nyumba ya kahaba mumoja aliyeitwa Rahabu wakalala humo. 2 Mufalme wa muji wa Yeriko akaambiwa: “Wanaume wawili Waisraeli wameingia katika muji leo usiku kwa kuipeleleza inchi.” 3 Mufalme wa Yeriko akatuma watu kwa Rahabu, akisema: “Uwatoshe inje watu waliokuja katika nyumba yako maana wamekuja kuipeleleza inchi yote.” 4 Lakini, yule mwanamuke alikuwa amekwisha kuwaficha watu hao wawili. Basi, akawaambia wajumbe hao: “Ni kweli kwamba hao watu walikuja kwangu, lakini mimi sikujua wametoka wapi. 5 Wakati wa kufunga mulango wa muji giza lilipoingia, hao watu waliondoka. Kule walikokwenda mimi sijui; muwafuate upesi nanyi mutawapata.” 6 Lakini Rahabu alikuwa amewapandisha hao wapelelezi juu ya dari na kuwaficha kwa vijiti vya kitani alivyokuwa ametandaza juu ya dari. 7 Basi, wale watu waliotumwa na mufalme wakawafuatilia kwa kupitia njia iliyokuwa imeelekea kwenye vivuko vya Yordani. Na mara tu walipoondoka katika muji, mulango wa muji ukafungwa. 8 Rahabu akawaendea hao wapelelezi juu kwenye dari mbele hawajalala, 9 akawaambia: “Mimi ninajua kwamba Yawe amewapa inchi hii; tumepatwa na hofu juu yenu na wakaaji wote wa inchi hii wanatetemeka kwa sababu yenu. 10 Maana tumesikia jinsi Yawe alivyoyakausha maji ya bahari Nyekundu mbele yenu mulipotoka inchi ya Misri, na jinsi mulivyowatendea wafalme wawili wa Waamori waliokuwa ngambo ya muto Yordani, ni kusema Sihoni na Ogi, ambao muliwaangamiza kabisa. 11 Mara tu tuliposikia mambo hayo, tukavunjika moyo kabisa kwa sababu yenu, tukaishiwa nguvu kabisa. Yawe, Mungu wenu, ndiye Mungu juu mbinguni na chini katika dunia! 12 Kwa hiyo basi, tafazali muniapie kwa jina la Yawe kwamba mutanitendea mema mimi na jamaa yangu kama vile mimi nilivyowatendea mema, na munipe uhakikisho kamili. 13 Muahidi kwamba mutamwacha baba yangu na mama yangu, kaka zangu na dada zangu, na jamaa yao yote; hamutakubali tuuawe!” 14 Wale watu wakamujibu: “Uzima wenu ni uzima wetu! Kama hamutaifichua siri yetu, Yawe atakapotupa inchi hii, tutakutendea kwa wema na uaminifu.” 15 Basi, Rahabu akawashusha hao watu kwa kamba kupitia katika dirisha: nyumba yake ilikuwa imejengwa ikiambatana na ukuta wa muji wa Yeriko. 16 Akawaambia: “Mwende kwenye mulima kusudi wale wanaowafuatilia wasiwakamate. Mujifiche kule kwa muda wa siku tatu, mpaka wale wanaowafuatilia watakapokuwa wamerudi katika muji. Kisha mutaweza kujiendea.” 17 Hao watu wakamwambia: “Sisi tutalitimiza kabisa jambo ulilotufanyia tunaahidi kwa kiapo. 18 Tutakapokuja katika inchi hii, funga kamba hii nyekundu kwenye dirisha ambalo umetuteremushia. Uwakusanye hapa kwako baba yako, mama yako na kaka zako na jamaa yote ya baba yako. 19 Lakini mutu yeyote akitoka inje ya nyumba yako na kwenda katika njia atabeba lazima ya kifo chake yeye mwenyewe. Lakini kama mutu yeyote atakayekuwa ndani ya nyumba yako akiguswa tu, basi lazima ya kifo chake itakuwa juu yetu. 20 Lakini kama ukimwambia mutu yeyote juu ya shuguli hii yetu, basi, sisi hatutatimiza kiapo ulichotuomba tukuapie.” 21 Naye akawaambia: “Ikuwe jinsi mulivyosema.” Kisha akawaruhusu waende zao, nao wakaondoka. Naye akaifunga ile kamba nyekundu kwenye dirisha. 22 Wapelelezi hao waliondoka wakaenda kwenye milima. Walikaa kule kwa muda wa siku tatu mpaka wale waliokuwa wanawafuatilia waliporudi katika muji Yeriko, nyuma ya kuwatafuta na kukosa kuwaona. 23 Basi, hao wapelelezi wawili wakashuka kutoka kwenye milima, wakavuka muto na kumwendea Yoshua mwana wa Nuni. Wakamwambia yote yaliyowapata. 24 Wakamwambia: “Hakika Yawe ameitia inchi yote katika mikono yetu. Tena wakaaji wa inchi hiyo wametetemeka kwa sababu yetu.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo