Muhubiri 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mashauri juu ya maisha 1 Sifa nzuri ni bora kuliko marasi ya bei kali. Siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa. 2 Afazali kwenda kwenye kilio, kuliko kwenda kwenye karamu, kwa sababu inawapasa wenye kuwa wazima kukumbuka kwamba kifo kinawangojea sisi wote. 3 Huzuni ni afazali kuliko kicheko, maana, kwa huzuni ya uso moyo unafurahishwa. 4 Moyo wa mwenye hekima uko ndani ya nyumba ya kilio, lakini moyo wa mupumbafu unapenda raha. 5 Afazali kusikia maonyo ya wenye hekima kuliko kusikiliza nyimbo za wapumbafu. 6 Maana, kicheko cha mupumbafu ni kama mulio wa miiba katika moto. Hayo nayo ni bure. 7 Mwenye hekima akimutesa mutu, yeye anafanya kama mupumbafu. Kupokea kituliro kunapotosha akili. 8 Mwisho wa jambo ni afazali kuliko mwanzo wake. Moyo muvumilivu ni bora kuliko moyo wa majivuno. 9 Usikuwe mwepesi wa hasira, maana, hasira inakaa ndani ya wapumbafu. 10 Usiulize: “Kwa nini nyakati za zamani zilikuwa bora kuliko za sasa?” Hauulizi hivyo kwa kutumia hekima. 11 Hekima ni ya bei kubwa kama urizi; ni ya mafaa kwa wale wote wanaokuwa wazima. 12 Kulindwa na hekima ni kama kulindwa na feza. Faida ya maarifa ni kwamba hekima inalinda maisha ya mutu anayekuwa nayo. 13 Mufikiri vema juu ya kazi ya Mungu. Ni nani anayeweza kunyoosha kitu Mungu alichokunja? 14 Katika siku za kufanikiwa ukuwe na furaha. Katika siku za hasara ufikiri juu ya jambo hili: Mungu amefanya hiyo ya kwanza iambatane na ya pili kusudi mwanadamu asipate kujua mambo yatakayotukia nyuma yake. 15 Katika maisha yangu ya bure, niliona kila kitu. Mutu wa haki anakufa ingawa ni wa haki, ambapo mutu mwovu anaendelea kuishi maisha marefu ingawa ni mwovu. 16 Basi, usikuwe wa haki kupita kipimo, wala usikuwe mwenye hekima zaidi! Kwa nini kujiangamiza wewe mwenyewe? 17 Lakini vilevile, usikuwe mwovu sana wala usikuwe mupumbafu! Kwa nini kufa mbele ya wakati wako? 18 Inakupasa ushike neno la kwanza na la pili vilevile; maana anayemutii Mungu atayaepuka yote. 19 Hekima inamufanya mwenye hekima kuwa na nguvu zaidi kuliko watawala kumi katika muji. 20 Hakika, hakuna mutu wa haki katika dunia anayetenda vizuri siku zote bila kutenda zambi. 21 Usifuate maneno yote wanadamu wanayosema, kusudi usisikie mutumishi wako akikutukana. 22 Wewe mwenyewe unajua ndani ya moyo kwamba umetukana wengine mara nyingi. Kuomba hekima 23 Nimeyapima yale yote kwa hekima; nikajisemesha: “Ninataka kuwa mwenye hekima!” Lakini hekima iko mbali sana nami. 24 Jinsi gani mwanadamu ataweza kutambua maana ya maisha? Jambo hilo ni zito na gumu sana kwetu. 25 Hata hivyo, nilikusudia kujua na kuchunguza na kutafuta hekima na maana ya mambo yanayokuwa, na vilevile kujua kwamba uovu ni upumbafu na kwamba upumbafu ni wazimu. 26 Jambo moja nililotambua linalokuwa baya zaidi kuliko kifo, ni mwanamuke ambaye moyo wake ni mutego na wavu, na mikono yake ni kama minyororo. Lakini anayemupendeza Mungu anamwepuka mwanamuke yule, lakini mwenye zambi ananaswa naye. 27 Ninakuambia mimi Muhubiri, haya ndiyo niliyotambua nilipofanya uchunguzi wangu kidogokidogo. 28 Niliendelea kutafuta mambo hayo, lakini sikupata. Kati ya wanaume elfu moja, nilipata kuona mwanaume mumoja anayestahili heshima, lakini kati ya wanawake wote, sikuona hata mumoja anayestahili heshima. 29 Nimetambua jambo hili moja: kwamba Mungu aliwaumba wanadamu wenye usawa, lakini wao wenyewe wamejitafutia matatizo. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo