Muhubiri 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Basi, nikawaza: “Ngoja nijitumbukize katika raha, nijifurahishe.” Lakini, niligundua kwamba hiyo nayo ni bure. 2 Nikasema juu ya kicheko: “Ni wazimu”, na raha: “Iko na faida gani?” 3 Nilitafuta kwa hekima namna ya kujichangamusha mwili kwa divai na kutenda sawa na wapumbafu. Nilitaka kuona kitu gani ni kizuri kwa wanadamu kufanya wanapoishi maisha yao mafupi hapa chini ya mbingu. 4 Nilifanya mambo makubwa: nilijenga nyumba na kujilimia mashamba ya mizabibu. 5 Nilijifanyia bustani na mashamba ya miti, nikapanda miti ya matunda ya kila aina. 6 Nilijichimbia visima vya maji ya kumwangilia ile miti. 7 Nilinunua watumwa, wajakazi, na wengine wakazaliwa katika nyumba yangu. Nilikuwa na mali mengi, makundi ya ngombe na kondoo wengi kuliko mutu yeyote aliyenitangulia kukaa Yerusalema. 8 Nilijikusanyia feza na zahabu kutoka hazina za wafalme na toka katika majimbo, nami nilipata waimbaji wanaume na wanawake, na wahabara wanaotamaniwa. 9 Nikakuwa mukubwa, mukubwa kuwapita wote waliopata kuwa katika Yerusalema mbele yangu. Na hekima yangu ikakaa ndani yangu. 10 Kila kitu macho yangu yalichokitamani nilikipata. Moyo wangu sikuunyima raha yoyote. Moyo wangu ulifurahia mambo niliyotenda, na hii ilikuwa zawadi ya jasho langu. 11 Kisha nikafikiri juu ya yote niliyokuwa nimefanya kwa mikono yangu, na jinsi nilivyotoa jasho kwa kuyafanya. Nikatambua kwamba yote ni bure sawa na kutaka kukamata upepo. Hakukukuwa faida yoyote chini ya jua. 12 Basi, nikaanza kufikiri maana ya kuwa na hekima, kuwa mwenda-wazimu, na kuwa mupumbafu. Nikajiuliza: “Mufalme mupya anaweza kufanya kitu gani? Atafanya tu kile kilichofanywa mbele yake.” 13 Basi, mimi nikagundua kwamba hekima ni bora kuliko upumbafu, kama vile mwangaza unavyokuwa bora kuliko giza. 14 Mwenye hekima anaona anakokwenda, lakini mupumbafu anatembea katika giza. Hata hivyo, ninajua vilevile kwamba mwisho wao wote wawili ni mumoja. 15 Basi, nikasema ndani ya moyo wangu: “Yatakayomupata mupumbafu yatanipata na mimi vilevile. Kwa nini, basi, nimekuwa na hekima zaidi?” Nikasema ndani ya moyo wangu: “Hayo nayo ni bure.” 16 Maana hakuna anayemukumbuka mwenye hekima, wala anayemukumbuka mupumbafu, maana katika siku zinazokuja wote watasahaulika. Maana mwenye hekima anakufa sawasawa na mupumbafu! 17 Kwa hiyo, nikachukia maisha, maana yote yanayotendeka chini ya jua yalinisikitisha. Yote ni bure sawa na kutaka kukamata upepo. 18 Nikachukia jasho yote niliyotoa hapa chini ya jua, kuona kwamba ilinipasa nimwachie mutu ambaye atatawala nyuma yangu. 19 Tena, ni nani anayejua kwamba atakuwa mwenye hekima au atakuwa mupumbafu? Hata hivyo, yeye atarizi yote niliyofanya kwa kutoa jasho na kutumia hekima yangu hapa chini ya jua. Hayo nayo ni bure. 20 Basi, nilipofikiri tena juu ya jasho yote niliyotoa chini ya jua, nilikata tamaa. 21 Maana, wakati mwingine, mutu ambaye amefanya kazi kwa kutumia hekima, akili na maarifa yake, anamwachia mutu mwingine afurahie matunda ya kazi ambayo hakuitoshea jasho. Hayo nayo ni bure. Ni jambo baya sana. 22 Mutu anafaidia nini kutokana na jasho yake yote, na juhudi anazohangaika nazo chini ya jua? 23 Maisha yake yote yamejaa taabu, na jasho yake ni mahangaiko matupu. Hata usiku akili yake haipumziki! Hayo nayo ni bure. 24 Hakuna kitu kizuri kwa mwanadamu, isipokuwa kula na kunywa na kufurahia matunda ya jasho yake. Hili nalo nimeliona kwamba linatoka kwa Mungu, 25 maana usipojaliwa na Mungu, hauwezi kupata chakula wala kujifurahisha. 26 Mungu anamujalia mutu anayependezwa naye hekima, akili na furaha; lakini anamupa mwenye zambi kazi ya kuvuna na kulundika, kisha Mungu anavipatia yule anayemupendeza. Hayo nayo ni bure sawa na kutaka kukamata upepo. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo