Muhubiri 11 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Jambo mwenye akili analopaswa kufanya 1 Tupa chakula chako juu ya maji. Nyuma ya siku nyingi utakipata tena! 2 Gawa sehemu moja kwa watu saba hata wanane, maana, haujui hasara itakayofika katika dunia. 3 Mawingu yakijaa maji, mvua inanyesha. Muti ukiangukia upande wa kusini au wa kaskazini, pale unapoangukia ndipo unapolala. 4 Anayechunguza upepo hatapanda mbegu, anayeangalia mawingu yatoweke, hatavuna kitu. 5 Kama vile hauwezi kujua jinsi uzima unavyoingia katika mifupa ya mutoto katika tumbo la mama yake, vilevile hauwezi kuelewa matendo ya Mungu, aliyefanya kila kitu. 6 Panda mbegu asubui na usiache kupanda mpaka magaribi, maana, haujui mbegu gani zitaota; za asubui, za magaribi, au zote zitakuwa nzuri. 7 Mwangaza ni muzuri, na kuona jua kunapendeza macho. 8 Mutu akiishi miaka mingi, afurahie miaka hiyo yote; lakini akumbuke kwamba siku mbaya zitakuwa nyingi, na kwamba yote yatakayofuata ni bure. Maonyo kwa vijana 9 Ewe kijana, furahia ujana wako, moyo wako ukuwe na raha wakati ungali kijana. Fuata mapenzi ya moyo wako na tamaa ya macho yako. Lakini kumbuka kwamba Mungu atakuhukumu kadiri ya hayo yote. 10 Ondoa mahangaiko ndani ya moyo wako, ujikinge usipate maumivu katika mwili kwa sababu ujana na nguvu vinapita mbio. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo